KUENDELEA MVUTANO WA KISIASA NCHINI ZIMBABWE

Kuendelea mvutano wa kisiasa nchini Zimbabwe
Zikiwa zimepita siku kadhaa tangu yalipojiri mapinduzi baridi ya kijeshi nchini Zimbabwe, wingu la mgogoro wa kisiasa lingali limetanda ndani ya nchi hiyo huku hatima ya mgogoro wenyewe ikibaki kuwa kitendawili.
Mgogoro wa kisiasa ulianza nchini Zimbabwe baada ya wapinzani wa Rais Robert Mugabe kulalamikia sera za kiongozi huyo hususan kuhusiana na uhuru wa kisiasa, kupambana na ufisadi na vilevile sera zake za kiuchumi. Uzee wa Mugabe mwenye umri wa miaka 93 na suala la atakayekuwa mrithi wake ni maudhui nyengine iliyozusha taharuki na kuzidisha mvutano wa kisiasa katika wiki za hivi karibuni nchini humo. Wapinzani walikuwa na wasiwasi juu ya njia isiyo ya kidemokrasia ambayo inaonekana Mugabe ametaka kuitumia kwa ajili ya kuainisha mrithi wake wa uongozi; na hasa kutokana na ushindani mkali ambao umekuwa ukiendelea kushuhudiwa kati ya mke wa Mugabe Grace na aliyekuwa makamu wa kiongozi huyo Emmerson Mnangagwa.
Rais Mugabe (katikati), Mnangagwa (kushoto) na Grace (kulia)
Wakati huohuo, wengi walikuwa wakitabiri kwamba Mnangagwa angekuwa ndiye mrithi wa Rais Mugabe katika mustakabali wa siasa za Zimbabwe, lakini siku kadhaa zilizopita, na katika hatua ambayo haikutarajiwa Mugabe alimuuzulu makamu wake huyo kwa kile alichodai kwamba ni kutokuwa na imani na utendaji wake na kutotekeleza majukumu yake ipasavyo. Hatua hiyo ya Rais wa Zimbabwe ilizidi kuipa nguvu dhana iliyokuwepo kuhusu mpango wa kumfanya mkewe Grace kuwa mrithi wa uongozi baada yake; na hata vyama vingi vya siasa viliitathmini hatua hiyo ya Mugabe kuwa ni uandaaji mazingira ya kumweka Bi Grace madarakani. Kufuatia kujitokeza kwa hali hiyo, jeshi liliingilia kati kwa kutuma magari ya deraya katika barabara za mji mkuu Harare, kuvishikilia vituo vya redio na televisheni za taifa na kumweka Mugabe mwenyewe kwenye kizuizi cha nyumbani.
Majenerali na makamanda wa jeshi la Zimbabwe 
Ijapokuwa jeshi limetangaza kuwa limechukua hatua hiyo kwa madhumuni ya kuwachukulia hatua wale liliowataja kama "wahalifu" waliomzunguka kiongozi huyo, ambao wamesababishia Zimbabwe madhara na hasara za kiuchumi na kijamii, lakini baada ya kupita siku chache tu tangu yalipojiri mapinduzi ya kijeshi inaonekana kuwa mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo umeingia kwenye awamu mpya.
Hivi sasa yameanza kufanyika mashauriano ndani ya nchi na kieneo juu ya suala hilo huku kukiwepo na dhana kadhaa ikiwemo ile inayofikiriwa na wengi kwamba Emmerson Mnangagwa, makamu wa rais aliyeuzuliwa ndiye atakayeshika hatamu za uongozi wa nchi. Kama hilo litajiri, bila ya shaka changamoto za kisiasa zitaendelea kushuhudiwa nchini Zimbabwe kwa sababu watu wengi wanamwona yeye kama mtu wa mkono wa kulia wa Mugabe na anayeshabihiana naye sana kwa sifa na tabia za kiuongozi. Vyama vya upinzani vinamtuhumu Mnangagwa kuwa alihusika katika ukandamizaji uliofanyika nchini humo hususan wakati wa uchaguzi, pamoja na wizi na uporaji wa utajiri wa taifa. Kwa hivyo inatabiriwa kwamba endapo atashika hatamu za uongozi, hatokuwa na uungaji mkono wa wananchi, zaidi ya kutawala kwa kutegemea nguvu za kijeshi.
Wilf Mbanga, mchambuzi wa masuala ya kisiasa analizungumzia suala hilo kwa kusema: "ikiwa Mnangagwa atakuwa ndiye atayechaguliwa, hakuna matumaini yoyote ya kutokea mabadiliko chanya nchini Zimbabwe".
Maandamano ya wananchi ya kumpinga Rais Mugabe
Kwa upande mwengine, mbali na jeshi, zaidi ya makundi 100 yanayojumuisha jumuiya na asasi za kiraia pamoja na viongozi wanaopinga serikali yametoa taarifa ya pamoja ya kumtaka Mugabe ang'atuke madarakani kwa amani, lakini hadi sasa kiongozi huyo amekataa kuachia madaraka na kukabidhi hatamu za uongozi. Kutokana na hali hiyo, baadhi ya wachambuzi wanahisi kwamba baada ya mashauriano, kuna uwezekano Mugabe akarejea tena madarakani kwa sharti la kubaki uongozini hadi utakapofanyika uchaguzi mkuu ujao.
Inavyoonekana, wanachokingojea kwa matarajio wananchi wa Zimbabwe ni kuandaliwa mazingira ya kufanyika uchaguzi huru na wa kidemokrasia nchini humo. Matumaini yao ni kuona kiongozi wa muda mrefu wa nchi hiyo anaondoka madarakani, kunaundwa serikali ya mpito na hatimaye baada ya miongo kadhaa, yanaandaliwa mazingira ya kufanyika uchaguzi katika anga huru na ya utulivu kwa kushirikisha wagombea wa vyama tofauti vya siasa vya nchi hiyo.../ 

0 comments: