CCM YAWAFUKUZA UANACHAMA SOPHIA SIMBA NA WENZAKE KADHAA

Sophia Simba

NA K-VIS BLOG,DODOMA
VIGOGO kadhaa wa Chama Cha Mapinduzi wamefukuzwa uanachama kuanzia leo Machi 11, 2017 na wengine kupewa onyo kali kufuatia vikao viwili nyeti vya chama hicho, Kamati Kuu ya CCM, (CC) na Halmashauri Kuu ya chama hicho, (NEC).
Kwa mujibu wa taarifa ya maamuzi ya kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM iliyopatikana kwa vyombo vya habari jioni hii, sababu  za kufukuzwa uanachama kwa wanachama hao zimeelezwa kuwa ni “makosa ya maadili kinyume na katiba na kanuni za uongozi na maadili za CCM.
Waluofukuzwa (kuvuliwa) uanachama ni pamoja na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM, (UWT), ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum katika bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sophia Simba, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Rashid Madabida, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Iringa, Jesca Msambatavangu, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mara, Christopher Sanya, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, na Erasto Izengo Kwilasa.
Aidha taarifa hiyo imetaja orodha ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, waliofukuzwa uanachama kuwa ni pamoja na Ally kheri Sumaye, kutoka wilaya ya Babati Mjini, na Mathias Erasto Manga, kutoka wilaya ya Arumeru.
Taarifa hiyo imesema, Wana CCM wengine waliopewa onyo kali ni pamoja na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ambaye pamoja na kupewa onyo kali anatakiwa kuomba radhi, Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Kigoma, Josephine Genzabuke wakati Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Dodoma, Alhaji Adam Kimbisa, yeye amesamehewa.
Wajumbe wengine wa NEC waliopewa onyo kali ni pamoja na Ali Mchumo, kutoka wilaya ya Kilwa, huku Ajili Mchumo, mjumbe wa NEC kutoka wilaya ya Tunduru, yeye amevuliwa uongozi, Hassan Mazala mjumbe wa nec kutoka wilaya ya Singida mjini yeye amevuliwa uongozi pia na ndugu Valerian Allen Buretta kutoka wilaya ya Kibaha vijijini naye pia ameachishwa uongozi.

Jesca Msambatavangu.
Christopher Sanya

0 comments: