STRATIJIA MPYA YA ISIS KATIKA AWAMU YA BAADA YA KUSAMBARATISHWA
Posted by khamisimussa77@gmail.com at 10:21 PM
Licha ya kumalizwa na kuangamizwa kijeshi
genge la kigaidi la Daesh (ISIS) lakini bado hatuwezi kusema kuwa
vitendo vyote vya genge hilo la wakufurishaji vimemalizika.
Kukombolewa mji wa al Bukamal
huko Deir ez-Zor Syria na mji wa Rawa huko al Anbar Iraq kuna maana ya
kuangamizwa kijeshi genge la kigaidi la Daesh lakini hakuna maana ya
kumalizika jinai za genge hilo. Kundi hilo la kigaidi limeshindwa katika
ndoto zake za kuunda khilafa lakini hapo hapo imeanza awamu mpya ya
vitendo vya kundi hilo ambayo ni kama vile kurejea ilikuweko huko nyuma.
Hivi sasa Daesh haina tena zile nguvu za
kuwashawishi watu kama ilivyokuwa mwaka 2014 na baadaye ambapo baadhi
ya watu wenye fikra finyu walivutika kujiunga kwa wingi na genge hilo.
Mgogoro mkubwa uliolikumba kundi la Daesh hivi sasa ni uchache wa
wanachama wake na kupoteza vyanzo vyake vya kifedha. Pamoja na hayo,
genge hilo linaendeleza jinai zake kwa shabaha ya kuvuruga tu mambo na
kutoruhusu raia waishi kwa usalama na bila ya hofu. Hivi sasa genge hilo
halifikirii tena kuteka ardhi na kuunda khilafa yake, bali lengo lake
ni kuzusha hofu tu na kujionyesha mbele ya watu kuwa bado lipo.
Katika awamu hii mpya, genge hilo
linafanya operesheni za kigaidi na miripuko ya hapa na pale. Si hayo tu
lakini pia linatumia mbinu zisizo za kawaida kama vile kuwavamia na
kuwakanyaga kwa gari watu kama ilivyotokezea mara kadhaa katika nchi za
Magharibi kama vile Marekani na nchini Uhispania.
Nukta nyingine hapa katika awamu hii
mpya ya mashambulizi ya genge la kigaidi la ISIS ni kuwa kundi hilo
linafanya mashambulizi yake kwa kutumia vijikundi kadhaa ambavyo tab'an
havina mguso sana na wala havina nia ya kuwa na eneo la kijiografia la
kiutawala. Mfano wa wazi wa vijikundi hivyo ni kundi la kigaidi
lililozuka hivi karibuni nchini Afghanistan na kufanya mashambulizi ya
kigaidi nchini humo. Kuna uwezekano pia kwamba kundi la Daesh limefikia
mapatano na baadhi ya vijikundi vya kigaidi kuendesha mashambulizi yao
katika maeneo tofauti duniani.
Suala jingine ni kwamba kuna uwezekano
pia wa kutokea mabadiliko katika maeneo ya kijiografia ya Daesh yaani
genge hilo la kigaidi kuhamishia vitendo vyake katika maeneo mengine ya
dunia. Ijapokuwa nchi kama Syria, Iraq na Yemen bado ni muhimu kwa genge
hilo, lakini vitendo vya kigaidi vya kundi hilo vimepungua katika nchi
hizo kutokana na kudhoofishwa sana na sasa limeaamua kuelekeza nguvu
zake katika maeneo mengine duniani hasa kaskazini mwa Afrika ikiwemo
nchini Libya, Somalia na Nigeria. Inavyoonekana ni kwamba nchi za
Kiarabu zinapaswa kuwa na wasiwasi zaidi hivi sasa kuliko wakati
mwingine wowote kwani kuna raia wengi wa nchi hizo waliojiunga na Daesh
katika miaka ya hivi karibuni na baada ya kusambaratishwa dola lao
waliloota kuliunda katika ardhi za Syria na Iraq, sasa raia hao hawana
njia nyingine isipokuwa kurejea walikotoka, wakiwa wameiva kwa fikra za
ukufurishaji na za kigaidi tena wakiwa wamepata mafunzo ya kijeshi. Si
hayo tu, lakini watu hao wanaugua maradhi ya kisaikolojia kutokana na
jinai za kutisha walizoziona na baadhi yao walizozifanya huko Syria na
Iraq. Watu hao ni hatari kubwa kwa nchi za Magharibi kwani mara zote
wako tayari kutenda jambo lolote lile. Ni kwa sababu hiyo ndio maana
wafuatiliaji wa mambo wakasema kuwa, si jambo lililo mbali kuona
vinaongezeka vitendo vya kigaidi ya genge la kigaidi la Daesh katika
nchi za Magharibi.
Nukta ya mwisho ya kuashiria hapa ni
kuwa, genge la kigaidi la ISIS limesambaratishwa kijeshi lakini fikra za
Kidaesh na za ukufurishaji bado zipo. Watu wenye fikra hizo bado ni
wengi na si katika eneo la Mashariki ya Kati tu, bali pia katika nchi za
Magharibi ambazo kimsingi ndizo zilizounda magenge hayo na kuyaunga
mkono kifedha na kijeshi ili kuuvuruga ulimwengu wa Kiislamu. Jambo hilo
linazidi kutia nguvu tahadhari zinazotolewa za kutokea mashambulio ya
kigaidi katika nchi za Ulaya na Marekani.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: