Jeshi la
Polisi mkoa wa Mbeya limeendelea kufanya misako, operesheni na doria
zenye tija katika maeneo mbalimbali ili kudhibiti uhalifu na wahalifu na
limekuwa likishirikiana na wananchi na wadau wengine katika jitihada
hizo za kukabiliana na uhalifu na wahalifu na kupata mafanikio makubwa
ikiwa ni pamoja na kupungua kwa matukio makubwa ya uhalifu. Mafanikio
yaliyopatikana katika Misako ni kama ifuatavyo:-
KUPATIKANA NA SILAHA [GOBOLE]
Mnamo
tarehe 07.01.2017 majira ya saa 16:30 jioni huko katika Kijiji cha
Mhwela, Kata ya Mswiswi, Tarafa ya Ilongo iliyopo mpakani mwa Wilaya ya
Kipolisi Mbalizi na Mbarali Mkoa wa Mbeya, askari Polisi wakiwa katika
msako walimkamata mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la JOHN NOAH [28]
mkazi wa Ilongo akiwa na silaha aina ya gobole yenye namba MB 2688
iliyokuwa imefukiwa kwenye shamba la migomba ambayo alikuwa anamiliki
kinyume cha sheria. Upelelezi unaendelea.
Aidha
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kukabiliana na matukio makubwa
ya uhalifu pamoja na wahalifu. Jitihada zinaendelea kwa kushirikiana na
wananchi kuhakikisha Mkoa wetu unakuwa mahala salama. Kumekuwa na
matukio 03 ya mauaji kama ifuatavyo:-
Mnamo
tarehe 07.01.2017 majira ya saa 12:30 mchana huko Kijiji na Kata ya
Ifumbo, Tarafa ya Kiwanja, Wilaya ya Chunya, Mkoa wa Mbeya, Watu wawili
wanaosadikiwa kuwa majambazi waliofahamika kwa majina ya 1. PASCHAL
SIMCHIMBA [29] Mkazi Kanga na 2. TEGEMEA HENUS [34] Mkazi wa Tete
waliuawa na wananchi walioamua kujichukulia sheria mkononi baada ya
kuvamia eneo la wachimbaji wadogo wa dhahabu wakiwa na silaha aina ya
Short gun iliyotengenezwa kienyeji kwa lengo la kufanya unyang’anyi na
ndipo walizidiwa nguvu na wananchi hao.
Inadaiwa
kuwa majambazi hao walikuwa watano huku wakiwa na silaha silaha aina ya
short gun iliyotengenezwa kienyeji ikiwa imekatwa mtutu na risasi
mbili ndani ya magazini. Aidha inadaiwa kuwa wakati wa tukio hilo risasi
zilizogoma kupiga ndipo walizidiwa nguvu na wananchi kisha kupigwa mawe
hadi kufa na kuchomwa moto.
Chanzo
cha tukio hilo ni kuwania mali katika kitongoji cha Kasangakanyika
ambalo wachimbaji wadogo hufanya shughuli za uchimbaji madini ya
dhahabu. Marehemu wote wawili walishawahi kushitakiwa na kosa la
unyang’anyi wa kutumia silaha mwaka 2013 na kufikishwa mahakamani na
kuhukumiwa kifungo cha miaka 30. Pia watuhumiwa hao walikata rufaa na
kuachiwa mwaka 2014. Watuhumiwa watatu walikimbia mara baada ya tukio
hilo juhudi za kuwatafuta zinaendelea.
Mnamo
tarehe 07.01.2017 majira ya saa 09:00 asubuhi huko katika Kijiji cha
Dimbwe kilichopo Kata ya Ulembo, Tarafa ya Isangati, Wilaya ya Kipolilsi
Mbalizi, Mkoa wa Mbeya, Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la VARENCY
POSTA [25] mkazi wa kijiji cha Dimbwe alifariki dunia akiwa anapatiwa
matibabu katika kituo cha afya Ilembo baada ya kuchomwa kitu chenye ncha
kali kichwani na mtu aliyefahamika kwa jina la MISIS EDWARD [33] mkazi
wa Dimbwe.
Inadaiwa
kuwa chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa mapenzi kutokana na binti wa
Mtuhumiwa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na marehemu. Inadaiwa kuwa
mtuhumiwa kabla ya kutenda kosa hilo alimvizia njiani marehemu akiwa
anatoka kuangalia mpira na kisha kumchoma kitu chenye ncha kali hali
iliyosababisha kutokwa damu nyingi na kupelekea kifo chake akiwa
anapatiwa matibabu. Mtuhumiwa amekamatwa. Mwili wa marehemu umefanyiwa
uchunguzi na kukabidhiwa ndugu kwa taratibu za mazishi.
Mnamo
tarehe 07.01.2017 majira ya saa 08:00 asubuhi huko Kijiji cha Ngolela,
Kata ya Ipinda, Tarafa ya Tembela, Wilaya ya Kyela, Mkoa wa Mbeya, Mtu
mmoja aliyefahamika kwa jina la NURU ROMAN @ MWANG’OLELA [35] Mkazi wa
Ubaruku Wilaya ya Mbarali na mwenyeji wa Bujela Kisale Wilaya ya Kyela
aliuawa kwa kupigwa mawe sehemu mbalimbali za mwili wake na kundi la
watu waliojichukulia sheria mkononi kwa tuhuma za wizi.
Katika
tukio hilo EDWIN SHURIMA [40] mkazi wa Ubaruku Mbarali ambaye alikuwa na
marehemu alijeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake na amelazwa
Hospitali ya Wilaya ya Kyela na hali yake inaendelea vizuri.
Awali
imeelezwa kwamba marehemu na majeruhi walifika kijijini hapo kutokea
Ubaruku Mbarali kwa nia ya kwenda kwa mganga wa kienyeji kutafuta
kizimba cha kilimo cha mpunga. Wakiwa bado wanasubiri huduma kwa mganga
huyo ndipo kundi la watu likawavamia wakiwatuhumu kuwa ni wezi.
Watuhumiwa
watatu wamekamatwa kufuatia tukio hilo ambao ni 1. OBETH AMLIKE [43]
Mwenyekiti wa kijiji cha Ngolela. 2. ITIKO KYOLO [64] mkazi wa Ngolela
na 3. RUTH MGUNDA [26] mkazi wa Ngolela. Katika eneo la tukio kumekutwa
shoka moja lenye damu, Mwili wa marehemu umefanyiwa uchunguzi na daktari
na kukabidhiwa ndugu kwa taratibu za mazishi. Upelelezi unaendelea.
WITO:
Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Mbeya Naibu Kamishna wa Polisi DHAHIRI A. KIDAVASHARI
anatoa wito kwa wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani ni
kinyume cha sheria na badala yake wawafikishe watuhumiwa wanaowakamatwa
kwa makosa mbalimbali katika mamlaka husika kwa hatua zaidi za kisheria.
Aidha Kamanda KIDAVASHARI anaendelea kutoa wito kwa wananchi kutoa
taarifa za uhalifu na wahalifu mapema kwa Jeshi la Polisi kwa hatua
zaidi za kisheria.
Imesainiwa na:
[DHAHIRI A. KIDAVASHARI – DCP]
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: