SISITIZO LA WAISLAMU WA NIGERIA LA KUACHILIWA HURU SHEIKH IBRAHIM ZAKZAKY

Wanaharakati wa jumuiya ya kiraia ya Nigeria wameitaka rasmi serikali ya nchi hiyo imuachilie huru Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria, Sheikh Ibrahim Zakzaky anayeshikiliwa na vyombo vya usalama vya nchi hiyo kwa karibu mwaka mmoja sasa.
Wanaharakati hao wametishia kwamba, endapo takwa la kisheria la mamilioni ya Waislamu wa Nigeria halitatekelezwa na serikali na vyombo vya usalama vya nchi hiyo katika kipindi cha wiki moja ijayo, basi kutafanyika maandamano katika kila kona ya nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika.
Katika miezi ya hivi karibuni Waislamu wengi nchini Nigeria, wakiwa na lengo la kulalamikia marufuku ya mikusanyiko yao katika majimbo ya kaskazini mwa nchi hiyo hususan Kaduna, wamekuwa wakifanya maandamano ya amani na kukusanyika mbele ya vituo vya serikali.
Juma lililopita, vyombo vya usalama vya Nigeria vilibomoa na kuharibu majengo ikiwemo misikiti na shule za Harakati ya Kiislamu ya Nigeria katika jimbo la Kaduna, hatua ambayo ilikabiliwa na malalamiko makubwa ya Waislamu wa nchi hiyo. Uvamizi wa askari usalama wa Nigeria dhidi ya Waislamu ulikwenda sambamba na shughuli ya kidini ya Arubaini ya Imam Hussein as.
Sheikh Ibrahim Zakzaky, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria
Waislamu wasiopungua 100 waliuawa shahidi katika shambulio hilo la jeshi la Nigeria. Ya'kub ambaye ni kaka wa Sheikh Zakzaky anaamini kwamba, hujuma ya jeshi la Nigeria dhidi ya taasisi za Waislamu katika jimbo la Kaduna ni njama yenye lengo la kusambaratisha athari za Harakati ya Kiislamu ya Nigeria. Kwa mtazamo huo, baadhi ya mamluki katika jeshi la Nigeria wana wasiwasi mkubwa kuhusu ushawishi mkubwa wa harakati hiyo ya Kiislamu katika fikra za waliowengi nchini Nigeria na barani Afrika kwa ujumla. Maadui wana hofu kubwa ya kuenea dini tukufu ya Kiislamu na wanaona kuwa, shughuli za Harakati ya Kiislamu ya Nigeria ambayo iko katika nchi yenye idadi kubwa zaidi ya watu barani Afrika, zitapelekea kuongezeka wafuasi wa dini hiyo tukufu.
Nyaraka zinaonyesha kuwa, baadhi ya viongozi wa Nigeria ambao fikra na mitazamo yao inaendana na mitazamo ya madola ya Magharibi kama Marekani, wameazimia kuchunga maslahi haramu ya Washington na waitifaki wake barani Afrika. Waitifaki wa Marekani kama Saudi Arabia na utawala haramu wa Israel wana matarajio kwamba, kuongezeka ushawishi na satuwa ya Washington kwa waitifaki wake wa Afrika kama Nigeria kutawaandalia uwanja mwafaka wa kisiasa watawala wa Riyadh na Tel Aviv katika nchi za Kiafrika.
Maandamano ya kutaka kuchililiwa huru Sheikh Ibrahim Zakzaky
Hivi sasa umepita takribani mwaka mmoja tangu Sheikh Ibrahim Zakzaky alipotiwa mbaroni na kushikiliwa korokoroni huku makundi ya kiraia nchini Nigeria yakipaza sauti kwa pamoja na Waislamu yakitaka kuachiliwa huru kiongozi huyo wa Harakati ya Kiislamu. Disemba mwaka jana, jeshi la Nigeria lilifanya shambulio katika Husseiniyyah ya Baqiyyatullah katika mji wa Zaria na kuwaua shahidi mamia ya wafuasi wa Sheikh Zakzaky. Shirika la Msamaha Duniani la Amnesty International likishirikiana na serikali ya jimbo la Kaduna iliandaa ripoti yenye kurasa 193 kuhusiana na shambulioa la kinyama la jeshi dhidi ya Waislamu mjini Zaria. Ripoti hiyo ilifichua kwamba, Waislamu 347 waliuawa kwa umati na kuzikwa katika kaburi la umati. Ripoti hiyo iliwabainishia Walimwengu ukubwa wa jinai za jeshi la Nigeria dhidi ya Waislamu hao.
Waislamu wa Nigeria ambao wanaunda asilimia kubwa ya wakazi milioni 180 wa nchi hiyo, wanataraji kupatiwa haki zao za kijamii. Takwa hilo bila shaka halionekani kuwa lisilo la kimantiki hasa kwa kuzingatia hali mbaya waliokuwa nayo Waislamu katika tawala za kidikteta za chama kimoja au utawala wa kijeshi katika miongo ya 80 na 90.
Filihali, jumuiya za kutetea haki za binadamu nazo zinaitaka serikali ya Nigeria imwachilie huru haraka iwezekanavyo Sheikh Ibrahim Zakzaky ambaye kwa mujibu wa baadhi ya duru, hali yake ya kiafya hairidhishi tangu jeshi lilipowashambulia Waislamu mjini Zaria Disemba mwaka jana na kumtia mbaroni kiongozi huyo akiwa amejeruhiwa vibaya. 
Sheikh Zakzaky baada ya kukamatwa na jeshi la Nigeria

0 comments: