KIONGOZI WA UPINZANI NCHINI ZAMBIA AKAMATWA NA POLISI

Polisi nchini Zambia imemtia mbaroni Hakainde Hichilema, kinara wa chama kikuu cha upinzani cha United Party for National Development.
Stephen Katuka, Katibu Mkuu wa chama cha upinzani cha UPND ameliambia shirika la habari la AFP kuwa, maafisa wa polisi walivamia makazi ya Hichilema na kumtia mbaroni bila kutoa maelezo yoyote kwa familia yake.
Katuka amekosoa vikali hatua ya polisi kumtia nguvuni kinara wa upinzani bila kutoa ufafanuzi wowote huku akitaja kama kitendo cha kinyama hatua ya polisi kuvamia makazi ya mwanasiasa huyo bila waranti na kisha kurusha mabomu ya kutoa machozi katika nyumba iliyokuwa na watoto wadogo.
Rais Edgar Lungu wa Zambia
Hata hivyo baadhi ya duru za usalama zimedokeza kuwa, Hichilema amekatwa kwa kuwa mwishoni mwa wiki alizuia msafara wa magari ya Rais Edgar Lungu, magharibi mwa nchi.
Ni vyema kukumbusha hapa kuwa, Oktoba mwaka jana, polisi ya Zambia iliwatia mbaroni Hichilema na Geoffrey Mwamba, Mkuu na Naibu Mkuu wa chama kikuu cha upinzani cha United Party for National Development kwa tuhuma za uchochezi.
Uchaguzi wa Rais uliofanyika mwezi Agosti mwaka jana huko Zambia ulikuwa wenye ushindani mkali kati ya Rais wa sasa wa nchi hiyo Edgar Lungu na mgombea wa upinzani Hakainde Hichilema ambaye alidai kuibiwa kura.

0 comments: