HOSPITALI YA MUFINDI YAPATA MSAADA WA VITI VYA KUBEBA WAGONJWA
Kaimu
Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Dk Goodluck Mlimbila alikijaribu
kusukuma moja kati ya viti 33 vilivyotolewa na asasi ya MUVIMA kwa ajili
ya hospitali ya wilaya ya Mufindi. Anayefurahi katikati ni mkurugenzi
mwenza wa MUVIMA, Albert Chalamila akipongezwa na Katibu wa Afya wa
Wilaya hiyo, Atupekisye Mwakifamba
Albert
Chalamila na baadhi ya wanahabari wakiangalia hali ilivyo ndani ya wodi
ya wazazi ya hospitali hiyo; hapa wanaonekana baadhi ya wajawazito
wanaolala chini kutokana na ukosefu wa vitanda.
Na Denis Mlowe,Mufindi
ASASI
ya Mufindi Vijana kwa Maendeleo (MUVIMA) imetoa msaada kwa hospitali ya
wilaya ya Mufindi yenye matatizo mbalimbali kwa lengo la kusaidia
kutoa huduma bora kwa kutoa viti 33 vya kubeba wagonjwa.
Akikabidhi
msaada huo hivi karibuni Kaimu Mkurugenzi wa MUVIMA, Albert Chalamila
alisema asasi yao imeguswa na kero mbalimbali zinazoikabili hospitali
hiyo na kwa kuanzia ililazimika kutafuta viti hivyo kwa lengo la
kusaidia hospitali hiyo yenye matatizo mbalimbali yanayofifisha utoaji
wa huduma bora za afya, zikiwemo zile za wajawazito na watoto,
Alisema
kwa msaada wa asasi ya kimataifa ya Rafiki Surgical Mission ya
Australia waliomba msaada huo baada kuomba msaada wa vitanda kwa ajili
ya hospitali hiyo hivyo vitanda 23 vimekwishawasili bandari ya Dar es
Salaam na tumeanza na viti vya kubeba wagonjwa.
Alisema
Mkurugenzi Mkuu wa MUVIMA, Cosato Chumi anaendelea na utaratibu wa
kuvitoa vitanda hivyo bandarini na mara baada ya shughuli hiyo
kukamilika vitakavifdhiwa kwa uongozi wa hospitali hiyo.
Kaimu
Mganga wa Hospitali ya Wilaya ya Mufindi, Dk Goodluck Mlimbila kwamba
vitapunguza adha waliyokuwa wanapata watoa huduma wa hospitali hiyo ya
kupokea na kubeba mikononi, wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo.
Akishukuru
kwa msaada huo, Dk Mlimbila alisema hospitali hiyo ina upungufu mkubwa
wa vifaa tiba na dawa na akalitaja eneo lenye tatizo zaidi kuwa ni lile
la huduma kwa mjamzito na watoto.
Alisema
katika kuboresha huduma za uzazi, jengo lenye uwezo wa kulaza
wajawazito zaidi ya 100 na lenye chumba cha upasuaji na kile cha
kuhifadhia watoto wanaozaliwa kabla ya muda lilijengwa katika hospitali
hiyo ambayo awali ilikuwa ikitumia jengo lenye uwezo wa kuweka vitanda
27 tu.
Alisema
msaada uliotolewa na MUVIMA una umuhimu mkubwa katika hospitali hiyo
kwani utarahisisha huduma za ubebaji wagonjwa kutoka eneo moja hadi
lingine na utapunguza idadi ya wajawazito wanaolala chini baada ya
vitanda vilivyoahidiwa kuwasili.
Naye
Katibu wa Afya wa wilaya hiyo, Atupakisye Mwakifamba aliwataka MUVIMA
na wadau wengi kujitokeza kuzimaliza kero za utoaji huduma zinazoikabili
hospitali hiyo na vituo vingine vingi vya huduma wilayani humo.
Mwakifamba
alisema pamoja na wilaya hiyo kuwa na idadi ya kuridhisha ya watoa
huduma wenye ujuzi, inakabiliwa na upungufu mkubwa wa vifaa tiba, dawa
na magari ya kubeba wagonjwa.
0 comments: