BARAZA IA USHIRIKIANO LA GHUBA YA UAJEMI LAKARIRI SIASA ZA PROPAGANDA CHAFU DHIDI YA IRAN

Katika kikao chake cha hivi karibuni mjini Manama huko Bahrain, Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi lilitangaza uamuzi wa kuanza ushirikiano wa kijeshi na mipango ya kistratijia kati ya nchi wanachama.
Ushirikiano huo na mipango ya kijeshi baina ya nchi za Kiarabu za Ghuba ya Uajemi si jambo jipya lakini swali linalojitokeza hapa ni kwamba, ni kwa nini kikao cha Manama kimepewa mazingatio maalumu katika vyombo vya habri ya kikanda na vya Uingereza?
kwa kiasi fulani taarifa iliyotolewa mwishoni mwa kikao cha Manama inatoa jibu la swali hilo. Taarifa hiyo imeituhumu Iran kuwa inaingilia masuala ya nchi za Ghuba ya Uajemi na kumefanyika jitihada za makusudi za kudumisha propaganda chafu dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu na kuiarifisha kuwa ni kituo kikuu cha vitisho vinavyolikabili eneo hilo.
Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi kwa miaka kadhaa sasa limekuwa likikariri madai yasiyo na msingi wowote dhidi ya Iran katika taarifa za mikutano na vikao vyake. Mwenendo huo umedumishwa katika kikao cha sasa cha baraza hilo kwa tofauti kwamba, mara hii uungaji mkono wa serikali ya London kwa kile Waziri Mkuu wa Uingereza,Theresa May alichokiita kuwa ni "hatua za hujuma za Tehran katika Ghuba ya Uajemi" umejumuishwa pia katika taarifa ya Manama.
Ni wazi kuwa lengo la uungaji mkono huo wa Uingereza ni kutayarisha mazingira ya kurejesha majeshi ya nchi hiyo katika eneo la Ghuba ya Uajemi. Inapasa kueleweka hapa kuwa, Uingereza imekuwepo katika eneo la Ghuba ya Uajemi kama nchi ya kikoloni kwa muda mrefu unaokaribia karne mbili na kimsingi sehemu kubwa ya hitilafu za mipaka na madai yasiyo na msingi kuhusu umiliki wa ardhi yanayotolewa na watawala wa kifalme wa nchi za Kiarabu za eneo hilo ni mirathi ya kipindi cha ukoloni wa Uingereza. Mbali na hayo, malengo ya Saudi Arabia katika mpango huo mzima yanatofautiana kidogo na yale ya Uingereza na inaonekana kuwa Riyadh inafuatilia malengo yake maalumu. Malengo hayo zaidi yanatokana na ushindani wenye uharibifu kwa ajili ya kuwa na satua na udhibiti katika nchi nyingine za eneo hilo. Ni kutokana na msimamo huo ndiyo maana Saudi Arabia daima imekuwa ikiitazama Iran kwa jicho la mshindani. Huu ni uhakika ambao hata Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza amekiri ukweli wake baada ya kukosoa utendaji wa Saudia katika eneo la Ghuba ya Uajemi katika msimamo unaoonekana kukinzana kwa kiasi fulani na ule wa Waziri Mkuu wa nchi hiyo Theresa May. Gazeti la The Guardian la Uingereza limeonesha mkanda wa video ambao ndani yake Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Boris Johnson amekosoa vikali siasa za Saudi Arabia katika eneo la Mashariki ya Kati japokuwa ukosoaji huo umeandamana na uungaji mkono wa serikali ya London kwa utawala wa kifalme wa Riyadh.
Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May akiwa na wakuu wa PGCC mjini Manama Bahrain 
Theresa May ni mwanamke wa kwanza na Waziri Mkuu wa kwanza wa Uingereza kushiriki katika kikao cha Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi na katika kikao hicho ametoa pendekezo la ushirikiano zaidi kwa ajili ya kuimarisha usalama wa kuwekeza katika masuala ya ulinzi na mafunzo ya kijeshi. Katika pendekezo hili pia kunaonekana aina fulani ya kubadilika siasa za Saudia Arabia na kujielekeza zaidi kwa nchi za Ulaya badala ya Marekani. Gazeti la El Pais la Uhispania limeandika kuwa: Saudi Arabia inataka kuimarisha zaidi uhusiano wake na nchi nyingine zisizo Marekani. hata hivyo ni wazi kuwa, maana nyingine ya kubadilika kwa mwelekeo huo wa Saudia ni mgongano ulipo baina ya maslahi ya Uingereza na Marekani hususan baada ya London kujiondoa katika Umoja wa Ulaya.
Bahrain ambayo ilikuwa mwenyeji wa kikao hicho tangu mwaka 2011 imekuwa ikikandamiza harakati ya amani ya wananchi ya kutaka mageuzi na kudai haki zao za kisheria ikisaidiwa na Saudi Arabia. Yumkini kwamba moja kati ya sababu za kubadili mwelekeo wa Saudi Arabia na waitifaki wake kama Imarati na Bahrain ni kutaka kufidia kushindwa kwao katika masuala mbalimbali ya Mashariki ya Kati.
Bi Theresa May Waziri Mkuu wa Uingereza akizungumza mjini Manama na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohamed Bin Rashid 
Kwa miaka mingi maafisa wa serikali ya Saudia walikuwa wakimimina mafuta katika masoko ya kimataifa kwa shabaha eti ya kuifanya Iran ifilisike. Hata sasa Riyadh inaonekana kurudi nyuma katika medani zote. kwani sasa Yemen imekuwa Vietnam kwa Saudi Arabia. Kusimama kidete kwa watu wa Yemen dhidi ya uvamizi wa Saudi Arabia na washirika wake kumeshusha hadhi na heshima ya Saudia kijeshi na kidiplomaia. Kwa msingi huo ili kufunika na kukimbia fedheha hiyo, Saudia na washirika wake wanakimbilia mwavuli wa kuitaja Iran kuwa ni tishio katika jumuiya za kimataifa.

0 comments: