Umoja na mshikamano baina ya Waislamu, majibu bora kwa watenda jinai
Habari kutoka katika ardhi za Palestina
zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni zinaonesha kushtadi jinai dhidi ya
Wapalestina na jambo hilo limelifanya kuwa la wajibu suala la kuleta
umoja na mshikamano haraka iwezekanavyo katika safu za Waislamu na
wapenda haki duniani, kwa ajili ya kupambana na Israel na kuilazimisha
ikomeshe jinai zake dhidi ya wananchi madhlumu wa Palestina.
Udharura huo umejitokeza katika
hali ambayo Waislamu hivi sasa wamo katika Wiki ya Umoja inayoadhimishwa
kwa mnasaba wa Maulid ya Bwana Mtume Muhammad SAW.
Matukio ya eneo la Mashariki ya Kati
katika kipindi cha miongo mitatu iliyopita yanaonesha kuwa, msamiati
mpya wa kisiasa ambao mhimili wake ni kupinga uvamizi na kuwaunga mkono
wanyonge duniani mbele ya ubeberu wa waistikbari; na ambao pia msingi
wake ni mafundisho matukufu ya dini ya Kiislamu; umeingia katika kamusi
ya misamiati ya kimataifa, kwa baraka za ushindi wa Mapinduzi ya
Kiislamu ya Iran. Ni jambo lililo wazi kwamba, iwapo kadhia ya
Palestina na kukaliwa kwa mabavu maeneo mbalimbali ya Palestina hususan
mji mtakatifu wa Baytul Muqaddas itafanywa kuwa maudhui kuu ya
kuunganisha nguvu za kupambana na mabeberu, bila ya shaka yoyote jambo
hilo litavunja kivitendo njama zote za waistikbari wanaofanya kila
wawezalo kujaribu kuififiliza kadhia ya Palestina. Wazayuni na waungaji
mkono wao wanatumia njama mbalimbali kuwasahaulisha walimwengu suala la
Palestina na kuficha jinai zinazofanywa na Israel dhidi ya taifa hilo
madhlumu. Njama yao kuu ni kujaribu kulifanya suala la Palestina kuwa
linahusiana na Wapalestina wenyewe tu au kwa zaidi linahusiana na
Waarabu na halihusiani kivyovyote vile na ulimwengu wa Kiislamu, ili kwa
njia hiyo wawapokonye Waislamu haki yao ya kupigania ukombozi wa maeneo
yao matakatifu ya Palestina.
Mkutano wa Wiki ya Umoja wa Kiislamu mjini Tehran
Aidha Wazayuni wanafanya mashambulizi ya
mtawalia dhidi ya Wapalestina ili kuwadhoofisha na kuendeleza siasa zao
za kupora ardhi za Wapalestina hao. Lakini njama zote hizo zimeshindwa
kutokana na kuwa macho wananchi wa Palestina kiasi kwamba siku ya
Jumatano, wakati idadi kubwa ya wanajeshi wa utawala wa Kizayuni
walipoingia kwenye kambi ya wakimbizi ya Shuafat (Sha'fat) kwa madai ya
kufanya mazoezi ya kijeshi, Wapalestina walisimama kidete na kupambana
vikali na wanajeshi hao vamizi wa Israel.
Hii ni katika hali ambayo, tangu ilipoanza Intifadha ya Quds mwezi
Oktoba 2015 hadi hivi sasa, Wapalestina 268 wameshauawa shahidi. Bila ya
shaka ni kwa kuzingatia hatari kama hizo ndio maana Ayatullah Khamenei,
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu akawa anasisitizia mara kwa
mara udharura wa kushikamana Waislamu na kulindwa malengo matukufu ya
taifa la Palestina. Ayatullah Khamenei amekuwa akisisitiza kuwa, iwapo
Wapalestina wataungana na iwapo Waislamu wengine watashirikiana na
Wapalestina hao walioungana katika kukabiliana na Wazayuni, basi utawala
wa Kizayuni wa Israel hauwezi kudumu kwa zaidi ya miaka 25 ijayo.
Nukta ya kutaamali hapa ni kwamba, njia
pekee ya kukomboa haki za taifa la Palestina na kuikoa Quds Tukufu ni
muqawama na mapambano kwani njia nyingine zote zilizobakia ni tasa na
hazina mwisho mwema. Hivyo uungaji mkono wa pande zote kwa wanapambano
wa Palestina inabidi iwe ndio ajenda kuu ya Waislamu wote na kila mpenda
haki duniani.
Quds, Kibla cha Kwanza cha Waislamu
Jambo jengine ambalo halipaswi
kusahauliwa ni kwamba mabeberu wanafanya njama za kuwashughulisha
Waislamu na migogoro ya ndani ili kuwasahaulisha kadhia ya
Palestina. Hivyo kukabiliana kwa pamoja na makundi ya wakufurishaji kama
vile Daesh na magenge mengine ya kigaidi ni wajibu wa kila mtu kwani
kinyume na hivyo, kuna hatari kadhia ya Palestina ikawekwa pembeni
kutokana na migogoro inayozushwa kila uchao na magenge hayo ya
kitakfiri.
Hivi sasa Waislamu wamo katika Wiki ya
Umoja, wiki ambayo ni fursa bora ya kuwaunganisha na kuwafanya wawe kitu
kimoja. Ni jambo lisilo na shaka hata kidogo kwamba, fursa hiyo inabidi
itumiwe vyema kuwakumbusha Waislamu kuwa kadhia yao kuu ni suala la
Palestina na kwamba magenge ya kigaidi na kitakfiri ni katika njama za
maadui wa Uislamu za kuwavunja nguvu Waislamu na kuwasahaulisha kadhia
yao kuu, yaani kupambana na Israel ambayo inayakaliwa kwa mabavu maeneo
yao matakatifu huko Palestina, ikiwemo Quds, ambacho ni Kibla cha Kwanza
cha Waislamu.
0 comments: