Watu wenye silaha wamewalenga wafanyakazi
wanne ambao ni wajumbe wa kamati ya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika
katika mji wa Nyala katikati mwa mkoa wa Darfur Kusini nchini Sudan.
Katika hujuma hiyo wafanyakazi hao wa UN wametekwa nyara na
mwingine mmoja kuuawa. Habari zaidi zinaarifu kuwa, watu watano
waliokuwa wamejifunga niqabu nyusoni mwao na wakitumia gari lisilokuwa
na namba za usajili, waliwazuia wafanyakazi hao akiwemo mwanamke mmoja
na kisha kuwateka nyara na kumuua mmoja wao. Chanzo kimoja cha kamati hiyo ya Umoja wa Mataifa kimenukuliwa
kikisema kuwa, tukio hilo limejiri karibu na chuo kidogo cha elimu na
viwanda mjini hapo Nyala wakati wafanyakazi hao walipokuwa njiani
kuelekea ofisi moja ya Umoja wa Mataifa katika eneo la Saqra, kaskazini
mashariki mwa mji huo. Kwa mujibu wa ripoti hiyo baada ya uvamizi huo,
washambuliaji walimmiminia risasi mwanamke miongoni mwa wafanyakazi hao
na kuondoka na wengine. Mkuu wa polisi mkoa wa Darfur Kusini
amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa, polisi wamejiweka
katika hali ya tahadhari ambapo wamefunga njia zote za kuingia na
kutoka mkoani hapo. Hadi sasa hakuna kundi lolote lililotangaza kuhusika
na hujuma hiyo.
0 comments: