Latest Articles

TAASISI YA OMDTZ YAWEZESHA KATA TANO KUWA NA MIPANGO YA KUKABILI MAFURIKO DAR ES SALAAM

  Na Mwandishi wetu – Dar es Salaam


Taasisi ya OpenMap Development Tanzania (OMDTZ) kwa kushirikiana na Serikali imeanza zoezi la kukabidhi Mipango ya Kata ya Kujiandaa na Kukabiliana na Mafuriko kwa jamii katika kata tano za Jiji la Dar es Salaam. 

Zoezi hilo la siku tano kuanzia tarehe 14 hadi 18 Septemba 2026 ambalo litaziwezesha Kata kupokea mpango na elimu kwa lengo la kuzijea uwezo wa kukabiliana na mafuriko endapo yatatokea katika maeneo yao.

Zoezi hilo linalotekelezwa kupitia Mradi wa “Ramani Zetu, Sauti Zetu”, unaofadhiliwa na Zayed Sustainability Prize, linahusisha Kata za Keko, Makurumila, Mabibo, Ubungo na Tabata, na linalenga kuwezesha jamii na viongozi kuwa na mipango na taarifa sahihi za maeneo yao kwa ajili ya maandalizi na mwitikio wa mafuriko.

Akifungua rasmi zoezi hilo katika Kata ya Keko, Diwani wa Kata hiyo Mheshimiwa Ismail Amanzi alieleza umuhimu wa mipango hiyo kutumika kama nyenzo ya vitendo katika kuimarisha maandalizi ya jamii na kupunguza athari za mafuriko.

“Zoezi hili limekuja wakati sahihi hivyo, ni vyema tukaitumia fursa hii kwa kuhakikisha elimu tunayopewa inafanyiwa kazi kwa vitendo ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa kwa kuzingatia athari za mafuriko katika maeneo yetu”, alisema mhe. Amanzi
Kwa upande wake Mkurugenzi wa OpenMap Development Tanzania, Bw. Innocent Maholi, amesema ushirikishwaji wa jamii katika kutambua maeneo hatarishi na kuweka taarifa hizo kwenye ramani ni hatua muhimu ya kuhakikisha wananchi wanakuwa sehemu ya kwanza ya maandalizi ya maafa.

“Lengo letu si kutengeneza ramani pekee, bali kuhakikisha taarifa hizo zinatumika na jamii katika kufanya maamuzi na kuchukua hatua kabla ya mafuriko kutokea,” amesema Maholi.
Alifafanua kuwa, kupitia mipango hiyo, wananchi wamewezeshwa kutambua maeneo hatarishi, njia salama za uhamishaji, maeneo ya mikusanyiko na hatua muhimu za kuchukua kabla na wakati wa mafuriko. Zoezi hilo pia linahusisha elimu kwa jamii kuhusu tahadhari za mapema, usafi wa mifereji na hatua za msingi za uokoaji.

Mradi wa “Ramani Zetu, Sauti Zetu” unalenga kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya mafuriko kupitia ramani shirikishi, mipango ya maandalizi ya maafa na matumizi ya taarifa za ndani za jamii katika kuchukua hatua za kupunguza vihatarishi.

Ikumbukwe kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu yenye dhamana ya kuratibu shughuli za Serikali ikiwemo ya masuala ya maafa nchini imeendelea kusisitiza umuhimu wa maandalizi ya mapema na ushirikiano kati ya Serikali na jamii katika kupunguza madhara yatokanayo na majanga, hususan wakati wa misimu ya mvua hasa kipindi hiki cha mvua za El Nino.
AWALI

OpenMap Development Tanzania (OMDTZ) ni taasisi inayolenga kutumia teknolojia ya ramani, taarifa za kijiografia na ushirikishwaji wa jamii katika kutambua na kupunguza vihatarishi vya majanga. Kupitia Mradi wa “Ramani Zetu, Sauti Zetu”, OMDTZ inashirikiana na Serikali na wadau mbalimbali kuwezesha jamii kutambua maeneo hatarishi, njia salama na rasilimali muhimu, pamoja na kuandaa mipango ya maandalizi na kukabiliana na mafuriko ili kuimarisha ustahimilivu wa jamii.






read more

WAZIRI MKUU DKT. MWIGULU NCHEMBA NA MAWAZIRI WATOA POLE KWA RAIS SAMIA

 

  Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, pamoja na Mawaziri, wakimfariji Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, nyumbani kwake Kizimkazi, Kusini Unguja, Zanzibar, tarehe 10 Septemba 2026, kufuatia kifo cha mume wake, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan, aliyefariki dunia tarehe 7 Septemba 2026.






read more

TAASISI YA SARATANI YA OCEAN ROAD YATUA KANDA YA NYANDA ZA JUU KUSINI

 



Na Mwandishi    Wetu - Mbeya
 
16/8/2027 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI)Dkt. Diwani Msemo amesema kukamilika kwa ujenzi wa Kituo cha Saratani ORCI Mbeya kutakuwa ni hatua muhimu katika kutimiza azma ya Serikali ya kusogeza huduma za kibingwa na kibobezi za saratani karibu na wananchi wa Nyanda za Juu Kusini na nchi jirani.


Dkt. Msemo amesema Serikali imewekeza takribani Shilingi bilioni 11 katika ujenzi wa kituo hicho ambacho kinatarajiwa kukamilika Januari 2027 na kuongeza uwezo wa kutoa huduma za uchunguzi, tiba na ufuatiliaji wa wagonjwa wa saratani katika ukanda huo.


Akizungumza wakati wa ziara ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya ORCI katika mradi huo jijini Mbeya, Dkt. Msemo amesema ujenzi wa vituo vya kikanda ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kupanua huduma za saratani nchini huku ORCI ikiwa na jukumu la kusaidia kusambaza huduma za kibingwa na kibobezi katika maeneo mbalimbali.


Amesema hatua hiyo inalenga kupunguza mzigo kwa wagonjwa wanaolazimika kusafiri umbali mrefu kwenda Dar es Salaam kupata huduma maalumu za saratani.


“Tunapopanua huduma hizi kwenda katika kanda, tunamsogezea huduma mgonjwa badala ya kumlazimisha mgonjwa kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma",  amesema Dkt. Msemo.


Kwa mujibu wa Dkt. Msemo kituo hicho kina umuhimu wa kimkakati zaidi kutokana na nafasi ya Mbeya kama lango la Tanzania kuelekea nchi za Malawi, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).


Amesema uwepo wa huduma za saratani katika eneo hilo utatoa fursa kwa wagonjwa kutoka nchi hizo jirani kupata huduma ndani ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini badala ya kusafiri hadi Dar es Salaam hatua ambayo pia inaweza kuchochea utalii wa tiba.


“Kituo hiki kitakuwa na nafasi kubwa katika kutoa huduma kwa Watanzania na pia wagonjwa kutoka nchi jirani. Hii ni fursa ya kuimarisha utalii wa tiba katika ukanda huu", amesema.


Dkt. Msemo amesema uwekezaji huo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kupanua huduma za saratani nchini huku akibainisha kuwa kupitia mpango wa kudhibiti saratani wa mwaka 2012, ORCI ilipewa jukumu la kusambaza huduma za kibingwa na kibobezi katika maeneo mbalimbali nchini.


Amesema hadi sasa Serikali imewekeza zaidi ya Shilingi bilioni 60 kupitia ORCI katika kuboresha miundombinu ya huduma za saratani, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uwezo wa nchi kukabiliana na ongezeko la mzigo wa ugonjwa huo.


Akizungumza katika ziara hiyo Mkurugenzi wa Tiba wa Wizara ya Afya Dkt. Hamad Nyembea, amesema saratani bado ni changamoto kubwa duniani na Tanzania.


Amesema takwimu za mwaka 2024 zinaonyesha kuwa takribani watu milioni 20 duniani waligundulika kuwa na saratani, huku milioni 9.7 wakipoteza maisha kutokana na ugonjwa huo.


Kwa Tanzania amesema inakadiriwa kuwa wagonjwa wapya wa saratani wanafikia takribani 45,000 kwa mwaka huku karibu 30,000 wakipoteza maisha kutokana na ugonjwa huo.


Dkt. Nyembea amesema sehemu ya saratani inaweza kuzuilika na nyingine kugundulika mapema hivyo Serikali inaendelea kuwekeza katika upanuzi wa huduma pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wa afya.


“Takribani asilimia 50 ya saratani zinaweza kuzuilika, na nyingine zinaweza kugundulika mapema”,  amesema.

Amesema uwepo wa vituo vya kikanda kama Mbeya utasaidia kuongeza upatikanaji wa huduma na kupunguza safari ndefu kwa wagonjwa, huku Serikali ikiendelea na mpango wa kujenga vituo vingine katika maeneo mbalimbali nchini.



Kwa mujibu wa Dkt. Nyembea kituo kingine cha saratani kinatarajiwa kuanza kujengwa Arusha  huku mipango ikiendelea kwa ajili ya vituo vya Kigoma na Mtwara.


Kwa upande wake Mkandarasi wa mradi huo, Ally Mtigita amesema ujenzi wa Kituo cha Saratani Mbeya ulianza mwaka 2024 na unatarajiwa kukamilika Januari mwaka 2027.


Amesema mradi huo wenye thamani ya takribani Shilingi bilioni 10.4 umefikia asilimia 57 ya utekelezaji huku kazi zikiendelea kwa kasi ili kuhakikisha kituo kinakamilika kwa wakati.

Kituo hicho kinatarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za uchunguzi, matibabu na ufuatiliaji wa wagonjwa wa saratani katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.


Uwekezaji huu unaashiria mabadiliko makubwa katika mfumo wa utoaji wa huduma za saratani nchini kutoka kutegemea zaidi vituo vichache vya kitaifa kuelekea mfumo wa huduma za kibingwa unaosogezwa karibu na wananchi.


Kituo cha Saratani cha ORCI  Mbeya kinapokamilika safari ya mgonjwa kutafuta huduma za saratani haitakuwa tena ndefu kama ilivyokuwa hapo awali; huduma zitakuwa karibu zaidi na matumaini ya kugundua na kutibu saratani mapema yataongezeka.

read more

MAKAMU WA RAIS DKT. NCHIMBI AMJULIA HALI MJANE WA RAIS WA KWANZA WA ZANZIBAR HAYATI SHEIKH ABEID AMANI KARUME

.  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemjulia hali, Mama Fatma Karume,Mjane wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, ambaye anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Lumumba Zanzibar.




 

read more

MAKAMU WA RAIS MHE. BALOZI NCHIMBI AMTEMBELEA SAIS MSTAAFU WA ZANZIBAR MHE. AMANI ABEID KARUME

  •    Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, Rais Mstaafu wa Zanzibar Mhe. Amani Abeid Karume, katika makazi yake, Mbweni - Unguja Zanzibar.




read more

RAIS SAMIA LEO AHITIMISHA TAMASHA LA KIZIMKAZI 2026

 

Kusini Unguja, Zanzibar 

Leo nimehitimisha Tamasha la Kizimkazi 2026, baada ya siku tatu za shangwe, fursa na shughuli mbalimbali zilizolenga kujenga umoja, kukuza fursa za biashara na uwekezaji, kutangaza utamaduni na utalii wetu, pamoja na kufungua miradi ya maendeleo kwa wananchi. Tunatarajia matokeo ya shughuli hizi kuendelea kuonekana hata baada ya tamasha kumalizika.

Ninawashukuru wote walioshiriki na kufanikisha tamasha hili. Ninawasihi tuendelee kushikamana, tudumishe amani, utulivu na usalama wa nchi yetu, kwa kuwa ndiyo msingi wa maendeleo na ustawi wetu.



read more

RAIS DKT. MWINYI: TAMASHA LA KIZIMKAZI NI JUKWAA LA UTAMADUNI, UTALII NA FURSA ZA UWEKEZAJI

  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tamasha la Kizimkazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utamaduni, utalii, biashara na fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar, sambamba na kuchochea maendeleo ya wananchi.


Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 12 Agosti 2026, alipokuwa akizindua rasmi Tamasha la Kizimkazi 2026 lenye kaulimbiu “KIZIMKAZI Kumenoga!” katika Mkoa wa Kusini Unguja.


Amepongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maono ya kuasisi Tamasha hilo, ambalo limekuwa likichangia kuhifadhi mila na utamaduni, kukuza utalii na kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi.


Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kutumia Tamasha hilo kutangaza fursa za uwekezaji katika utalii, uvuvi, mwani na Uchumi wa Buluu, huku Serikali ikiendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji na miundombinu ya uzalishaji.


Amesema Tamasha la Kizimkazi linaunga mkono dhamira ya Serikali ya kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Zanzibar kutoka 800,000 hadi milioni 1.5, kupitia matukio maalum ya utalii na utangazaji wa vivutio, utamaduni, vyakula na ukarimu wa Wazanzibari.


Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza waandaaji, wadhamini, taasisi za Serikali, Sekta Binafsi, wajasiriamali, wasanii, wanamichezo na wananchi kwa kufanikisha Tamasha la Kizimkazi 2026, akihimiza kuendelea kulitumia kama jukwaa la kufungua fursa mpya za maendeleo.

Tamasha hilo linaendelea hadi tarehe 14 Agosti 2026, ambapo kilele chake kitafanyika katika Uwanja wa Mwehe, Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja.

















read more