Latest Articles

WAZAZI WAHIMIZWA KUWACHANJA WATOTO KINGA YA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI

Watumishi wa Wizara ya Fedha wakimsikiza Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Frank Rutachunzibwa wakati akitoa elimu ya magonjwa ya saratani kwenye zoezi la upimaji afya linalofanyika kwa wafanyakazi hao Mtumba jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mali za Serikali kutoka Wizara ya Fedha, Choto Sendo akiuliza swali kuhusu magonjwa ya saratani wakati wa zoezi la upimaji afya linalofanywa na waatalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI)  kwa watumishi wa wizara hiyo iliyopo Mtumba jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Kinga wa  Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Crispin Kahesa , akitoa elimu ya magonjwa ya Saratani kwa watumishi wa Wizara ya Fedha wakati wa zoezi la upimaji afya linalofanyika kwa watumishi hao Mtumba jijini Dodoma
Watumishi wa Wizara ya Fedha wakimsikiza Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Frank Rutachunzibwa wakati akitoa elimu ya magonjwa ya saratani kwenye zoezi la upimaji afya linalofanyika kwa wafanyakazi hao Mtumba jijini Dodoma.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Frank Rutachunzibwa, akieleza umuhimu wa chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi kwa watoto wa kike wenye umri wa miaka 9 hadi 14  wakati wa zoezi la upimaji afya linalofanyika kwa Watumishi wa Wizara ya Fedha iliyopo Mtumba jijini Dodoma


Na Mwandishi wetu – Dodoma

10/08/2026 Wazazi na walezi nchini wametakiwa kuwapeleka watoto wao wa kike wenye umri wa miaka 9 hadi 14 kupata chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi ili kuwakinga dhidi ya ugonjwa huo unaoongoza kwa vifo miongoni mwa saratani za uzazi kwa wanawake.


Rai hiyo imetolewa leo na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Frank Rutachunzibwa, wakati akitoa mada ya uelimishaji kuhusu saratani kwa watumishi wa Wizara ya Fedha, Mtumba jijini Dodoma.


Dkt.Rutachunzibwa alisema chanjo hiyo hufanya kazi vizuri zaidi kwa watoto ambao bado hawajaanza kujamiiana kwani huwapa kinga dhidi ya maambukizi yanayoweza kusababisha saratani ya mlango wa kizazi baadaye katika maishani yao.

Alibainisha kuwa kila mwaka maelfu ya wanawake hupoteza maisha kutokana na saratani hiyo huku sababu kubwa ikiwa ni kuchelewa kugundua ugonjwa huo. 
“Kati ya wagonjwa wengi tunaowaona, idadi kubwa hufika hospitalini wakiwa katika hatua za mwisho” alisema.


Dkt. Frank Rutachunzibwa aliongeza kuwa pamoja na saratani ya mlango wa kizazi, zipo pia saratani nyingine zinazowaathiri watanzania wengi ikiwemo saratani ya matiti, tezi dume na mfumo wa chakula.

Daktati huyo Bingwa wa Magonjwa ya Saratani alisisitiza umuhimu wa kujichunguza  mapema na kufika hospitalini mara kwa mara kwa uchunguzi huku akionya kuwa watu wengi bado wanakimbilia tiba mbadala badala ya matibabu ya kisasa.


“Saratani inatibika kama magonjwa mengine. Ni muhimu kujipenda, kujichunguza na kutafuta matibabu sahihi bila kuchelewa lakini bado kuna imani potofu na mwitikio mdogo wa huduma za kinga, hali inayochangia wagonjwa wengi kugundulika katika hatua za mwisho za ugonjwa”, alisisitiza.


Alitaja baadhi ya vihatarishi vya saratani kuwa ni pamoja na mtindo usiofaa wa maisha, uvutaji wa sigara, pamoja na sababu za kinasaba. Pia alibainisha kuwa wanaume wanaweza kupata saratani ya matiti ingawa ni kwa kiwango kidogo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mali za Serikali, Choto Sendo aliishukuru Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) kwa kutoa elimu ya magonjwa ya saratani na yasiyo ya kuambukiza kwa watumishi wa Wizara hiyo na kusema kuwa elimu waliyoipata pamoja na upimaji watakaofanyiwa utawasaidia kujua hali za afya zao.


“Ninaishauri ORCI kuendelea kufanya tafiti ili kubaini sababu za ongezeko la saratani katika baadhi ya maeneo ya nchi, ikiwemo Kanda ya kaskazini ,Nyanda za juu kusini, Kanda ya Ziwa na Dar es Salaam, ni muhimu kuelewa chanzo cha tatizo ili kuweka mikakati madhubuti ya kinga badala ya kuendelea kutoa matibabu pekee”, alisema Sendo.


Saratani ya mlango wa kizazi ni miongoni mwa saratani zinazoongoza kwa vifo vya wanawake nchini, huku changamoto kubwa ikiwa ni uelewa mdogo na kuchelewa kwa uchunguzi na matibabu. Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, chanjo kwa watoto wa umri wa miaka 9 hadi 14 ni njia muhimu ya kinga dhidi ya ugonjwa huo sambamba na uchunguzi wa mara kwa mara kwa watu wazima. 
read more

MAKAMU WA RAIS DKT NCHIMBI AMJULIA HALI RAIS MSTAAFU DKT.KIKWETE NYUMBANI KWAKE

 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, katika makazi yake, Kawe Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 10 Agosti 2026.




read more

RAIS MWINYI AFANYA UTEUZI



 

read more

RAIS SAMIA AUNGANA NA VIONGOZI WENGINE KUFUNGUA MKUTANO MKUU WA WANAHISA

 

Leo jijini Dar es Salaam nimeungana na viongozi wengine wa Afrika kufungua Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Taasisi ya Africa50 na Jukwaa la Miundombinu Afrika, ambapo Tanzania imepata heshima ya kuwa mwenyeji. Jukwaa hilo, linaloadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake, limekuwa sehemu muhimu ya kuunganisha mitaji, miradi na wataalamu ili kuharakisha maendeleo ya miundombinu barani Afrika.


Katika mkutano huo nimeeleza kuwa, Tanzania inashirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kuimarisha miundombinu, ikiwemo barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege. Hatua hii inachochea ukuaji endelevu wa uchumi kwa kupunguza gharama za usafirishaji, kukuza biashara, kuvutia uwekezaji, kutoa ajira na kuifanya nchi yetu kuwa kitovu cha usafirishaji.


Kutokana na mabadiliko ya kiuchumi, kisiasa na kimazingira duniani, nimesisitiza umuhimu wa Afrika kuimarisha miundombinu inayohimili mabadiliko hayo na kuunganisha nchi zetu ili kuendelea kukuza biashara, uwekezaji na uongezaji thamani wa rasilimali zetu.



read more

MHE. KIKWETE ASISITIZA UMUHIMU WA UMMA KUPIMA AFYA MARA KWA MARA

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akipokea mfuko wenye vipeperushi vya elimu ya magonjwa ya Saratani kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Dkt. Diwani Msemo wakati wa zoezi la upimaji wa afya kwa watumishi wa ofisi hiyo linalofanyika Mtumba jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Prisca Lwangili akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Dkt. Diwani Msemo wakati Naibu Katibu Mkuu huyo alipowasili katika Ofisi hizo zilizopo Mtumba jijini Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa ofisi hiyo pamoja na wataalamu wa afya kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) wataalamu wa ORCI wanatoa huduma ya upimaji wa afya kwa watumishi wa Ofisi hiyo iliyopo Mtumba jijini Dodoma.
   Afisa Muuguzi kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Sonica Gennis akigawa vipeperushi vya elimu ya magonjwa ya Saratani kwa watumishi wa Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati wa zoezi la upimaji wa afya linalofanyika Mtumba jijini Dodoma. 


Na Mwandishi wetu– Dodoma


05/08/2026 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka watumishi wa wizara hiyo kujenga utamaduni wa kupima afya zao mara kwa mara ili kujikinga na magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo ya kansa yanayoweza kutibika kama yakigundulika mapema.


Mhe. Kikwete ametoa kauli hiyo leo wakati wa zoezi la upimaji wa magonjwa ya Saratani na yasiyo ya kuambukiza linalofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) kwa watumishi wa ofisi hiyo iliyopo Mtumba jijini Dodoma. 


Mhe. Kikwete alisema zoezi hilo ni fursa muhimu kwa watumishi hao kujua hali zao za afya huku akibainisha kuwa wengi wao hukosa muda wa kwenda kupima kutokana na majukumu ya kazi.


“Leo hii wataalamu kutoka Hospitali ya Ocean Road wamekuja hapa kutupima magonjwa ya saratani na yasiyo ya kuambukiza. Ni muhimu kutumia fursa hii kupima afya kwani ukigundulika na changamoto yoyote mapema utaweza kupata matibabu kwa wakati”, alisisitiza.


Mhe. Kikwete aliwashukuru wataalamu wa ORCI kwa kuwafikia watumishi mahali pa kazi hatua hiyo ni kielelezo cha dhamira ya Serikali katika kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi na wafanyakazi wake popote walipo.


Alitoa wito kwa taasisi hiyo kuendelea kusambaza huduma hizo katika maeneo mengine ikiwemo ngazi za wilaya ili kuwafikia watumishi wengi zaidi ambao muda mwingi hutumia kazini na kukosa nafasi ya kwenda hospitali kupima afya.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Diwani Msemo alisema taasisi hiyo imekuwa ikitoa huduma za uchunguzi wa afya katika maeneo mbalimbali nchini ambapo hadi sasa imefikia mikoa 15 na kuhudumia zaidi ya watu 200,000 kupitia programu ya Huduma Mkoba.


Dkt. Msemo ambaye pia ni Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Saratani alieleza kuwa huduma zinazowafuata watumishi mahali pa kazi zimekuwa na mwitikio mkubwa akibainisha kuwa katika ofisi hiyo kwa mud awa siku tatu wamefanikiwa kupima takribani watumishi 200.


Aliongeza kuwa kuchelewa kugundua magonjwa kama Saratani kunafanya matibabu kuwa magumu zaidi hivyo kusisitiza umuhimu wa watu kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.


Nao baadhi ya watumishi waliopata huduma za uchunguzi wa afya waliushukuru uongozi wa Ofisi hiyo kwa kuwaletea huduma za uchunguzi wa afya mahali walipo na kueleza kuridhishwa na zoezi hilo huku wakisema limewasaidia kutambua hali zao za afya na kuchukua hatua stahiki.


Deus Kimaro alisema huduma hiyo imewapa urahisi wa kupima afya bila kuathiri majukumu yao ya kazi kwani siku ya Jumatatu walipata mafunzo ya Saratani na magonjwa yasiyo ya kuambukiza yaliyokwenda sambamba na huduma ya upimaji ambayo inafanyika kwa muda wa siku tano.


“Huduma zilizotolewa ni bora na zimetupa fursa ya kujua hali zetu za afya mapema, watumishi wengi wamejitokeza kupima tunaomba huduma hizi ziendelee kusambazwa zaidi katika maeneo mbalimbali ya nchi ili kuwafikia watu wengi zaidi”, alisema Hawa Mgong’oli Afisa Utawala Mkuu. 


Zoezi hilo linaendelea kuwa sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha watumishi wa umma wanakuwa na afya bora hali itakayowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya taifa. 

Na Mpiga picha wetu

read more

OCEAN ROAD NA MUHIMBILI WAWEKA MIKAKATI YA KUBORESHA HUDUMA ZA KINGA, UCHUNGUZI, MATIBABU NA UFUATILIAJI WA WAGONJWA WA SARATANI


 Na Mwandishi wetu


Katika hatua muhimu ya kuimarisha mapambano dhidi ya saratani nchini wataalamu wa afya kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wamekutana jijini Dar es Salaam kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha huduma za kinga, uchunguzi, matibabu na ufuatiliaji wa wagonjwa wa saratani.


Kikao hicho kilichoongozwa jana na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba wa ORCI, Dkt. Mark Mseti ni hatua ya kimkakati itakayochochea mageuzi ya utoaji huduma za saratani kwa kuongeza ufanisi, ubora na upatikanaji wa huduma hizo kwa wananchi.



Akizungumza kuhusu kikao hicho Dkt. Mseti alisema ushirikiano wa karibu kati ya ORCI na MNH ni muhimu katika kuhakikisha wagonjwa wanapata huduma stahiki kwa wakati huku akibainisha kuwa mikakati iliyowekwa inalenga kuimarisha uratibu wa huduma, kuboresha mifumo ya rufaa na mapokezi ya wagonjwa pamoja na kuongeza matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchunguzi na matibabu.



“Tunajenga mfumo imara utakaorahisisha huduma kuanzia uchunguzi hadi matibabu na ufuatiliaji huku tukihakikisha wataalamu wetu wanaendelea kujengewa uwezo kupitia mafunzo na kubadilishana uzoefu”, alisema Dkt. Mseti.



Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tiba wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Dkt. Faraja Chiwanga alisema ushirikiano huo unaimarisha zaidi uwezo wa taasisi hizo katika kutoa huduma bora kwa wagonjwa huku ukichochea matumizi sahihi ya rasilimali zilizopo.



Dkt. Chiwanga aliongeza kuwa juhudi hizo zinaweka msingi imara wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma za saratani zenye viwango vya juu zinazokidhi mahitaji yao na zinazokwenda sambamba na maendeleo ya teknolojia ya tiba duniani.



Kikao hicho kimejadili changamoto mbalimbali zinazoathiri utoaji wa huduma za saratani na kuweka mikakati ya kuzitatua ili kuhakikisha wagonjwa wanahudumiwa kwa viwango vya juu vya ubora, usalama na kwa wakati. Msisitizo pia umewekwa katika kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

read more

DKT. NCHIMBI AAGIZA UKAGUZI WA MARA KWA MARA KWA VYAMA VYA USHIRIKA, ATAKA UBADHIRIFU UKOMESHWE

 Na Mwandishi wetu - MichuziTv


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ameielekeza Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuimarisha ukaguzi wa mara kwa mara katika vyama vya ushirika nchini ili kudhibiti ubadhirifu wa mali, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha vyama hivyo vinatoa huduma bora kwa wanachama wake.


Dkt. Nchimbi amesema Serikali imejipanga kuifanya sekta ya ushirika kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kilimo na uchumi wa taifa kwa kuhakikisha mali za vyama vya ushirika zinalindwa, zinasimamiwa kwa ufanisi na zinatumika kwa manufaa ya wakulima na wanachama wote.


Amesema ukaguzi wa mara kwa mara utasaidia kubaini mapema changamoto zinazojitokeza katika vyama vya ushirika, hivyo kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa kabla ya kusababisha hasara au matumizi yasiyo sahihi ya rasilimali za wanachama.


Aidha, Dkt. Nchimbi amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowezesha vyama vya ushirika kuimarika zaidi ili viweze kuongeza mchango wake katika kuinua uzalishaji wa kilimo, kuongeza kipato cha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.


Ameeleza kuwa kwa sasa Tanzania ina vyama vya ushirika 2,531 ambavyo vinaendelea kuwa daraja muhimu la kuwafikishia wananchi huduma mbalimbali, hususan katika sekta ya kilimo, na kusisitiza kuwa vinapaswa kuendelea kuimarishwa ili viendane na mahitaji ya maendeleo ya nchi.


"Vyama vya ushirika vina nafasi kubwa katika maendeleo ya wananchi. Tunapaswa kuviwezesha na kuviimarisha ili viweze kutoa huduma bora zaidi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi," amesema Dkt. Nchimbi.


Pia amepongeza mafanikio yaliyopatikana katika sekta hiyo, akibainisha kuwa thamani ya biashara iliyofanywa kupitia vyama vya ushirika imeongezeka kutoka Sh trilioni 4.2 hadi kufikia Sh trilioni 4.9 katika msimu wa mwaka 2025/2026.


Ameongeza kuwa upatikanaji wa mitaji ni msingi muhimu wa kuimarisha uwekezaji katika sekta ya kilimo, hivyo Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wakulima wanapata fursa za kifedha zitakazowawezesha kuongeza uzalishaji na thamani ya mazao yao.


Kwa upande wake, Mrajisi wa Vyama vya Ushirika, Benson Ndiege, amesema Tume ya Maendeleo ya Ushirika imeanzisha mfumo maalumu wa kutambua na kuhakiki mali zinazomilikiwa na vyama vya ushirika nchini kwa lengo la kuwa na taarifa sahihi zitakazorahisisha usimamizi na matumizi yake.


Amesema mfumo huo utawezesha kujua thamani halisi ya mali za vyama vya ushirika, kuboresha utoaji wa huduma kwa wanachama na kuongeza uwazi katika usimamizi wa rasilimali za vyama hivyo.


Ndiege amesema hadi sasa mali 5,558 za vyama vya ushirika zimetambuliwa na kufanyiwa tathmini, zikiwa na thamani ya Sh milioni 18.6, huku akisisitiza kuwa zoezi hilo litaendelea sambamba na ukaguzi wa mara kwa mara ili kuhakikisha sheria, kanuni na taratibu za ushirika zinafuatwa.


Aidha, ametoa wito kwa wanachama na wadau wa sekta ya ushirika kushirikiana na Tume kwa kutoa taarifa na ushirikiano utakaosaidia kulinda mali za vyama hivyo na kuimarisha utendaji wake.


Naye Waziri wa Kilimo, Godfrey Chongolo, amesema Serikali itaendelea kuifanya sekta ya ushirika kuwa sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuhakikisha vyama vya ushirika vinaendeshwa kwa misingi ya uwazi, ufanisi na uwajibikaji.


Amesema Wizara ya Kilimo itaendelea kuhamasisha wananchi kujiunga na vyama vya ushirika vinavyofanya kazi kwa kuzingatia sheria, huku ikichukua hatua kali za kisheria dhidi ya wote watakaobainika kukiuka misingi na taratibu za ushirika.






read more