Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Frank Rutachunzibwa, akitoa elimu kuhusu mionzi tiba ya saratani kwa wafanyakazi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati timu ya wataalamu kutoka ORCI ilipofika katika ofisi hizo zilizopo Mtumba jijini Dodoma kwaajili ya kutoa huduma za upimaji wa saratani na magonjwa yasiyoambukiza.
Mtumishi kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Rukia Hussein akiuliza swali kuhusu chanjo ya saratani ya kizazi wakati wataalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) walipofika katika ofisi hizo zilizopo Mtumba jijini Dodoma kutoa elimu pamoja na huduma za upimaji wa saratani na magonjwa yasiyoambukiza.
Mtumishi kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Thobias Setumbi akiuliza swali kuhusu chanjo ya saratani ya kizazi wakati wataalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) walipofika katika ofisi hizo zilizopo Mtumba jijini Dodoma kwaajili ya kutoa elimu pamoja na huduma za upimaji wa saratani na magonjwa yasiyoambukiza.
Afisa Rasilimali Watu Mkuu kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Innocent Kessy akiuliza swali kuhusu magonjwa ya saratani wakati wataalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) walipofika katika ofisi hizo zilizopo Mtumba jijini Dodoma kutoa elimu pamoja na huduma za upimaji wa saratani na magonjwa yasiyoambukiza.
Na Mwandishi Maalumu - Dodoma
03/08/2026 Wanaume wametakiwa kujitokeza kupima saratani ya matiti mapema licha ya dhana iliyozoeleka kuwa ugonjwa huo huwapata wanawake pekee lakini wanaume pia wako katika hatari ya kuugua saratani hiyo ingawa kwa kiwango kidogo.
Wito huo umetolewa leo na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Dkt. Maguha Stephano wakati akitoa elimu kuhusu saratani na magonjwa yasiyoambukiza kwa wafanyakazi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora jijini Dodoma.
Zoezi hilo la utoaji wa elimu ya magonjwa ya saratani linaenda sambamba na upimaji wa saratani pamoja na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa wafanyakazi hao.
Dkt. Maguha alieleza kuwa saratani ya matiti kwa wanawake huchangia takribani asilimia 99 ya visa vyote vya saratani ya matiti Tanzania huku wanaume wakichangia asilimia 1. Hata hivyo alibainisha kuwa uelewa mdogo miongoni mwa wanaume husababisha wengi wao kugundulika wakiwa katika hatua za mwisho za ugonjwa.
“Wanaume pia wanapata saratani ya matiti, lakini wengi hawajitokezi kupima mapema kutokana na kukosa uelewa. Hii husababisha ugonjwa kugundulika ukiwa umefikia hatua ya juu”, alisema Dkt. Maguha.
Alifafanua kuwa kadri umri unavyoongezeka ndivyo hatari ya kupata saratani inavyoongezeka. Alitaja visababishi vya ugonjwa huo kuwa ni pamoja na kurithi, matumizi ya kemikali hatarishi, kutokufanya mazoezi, matumizi ya tumbaku na bidhaa zake pamoja na lishe isiyo bora.
Akizungumzia dalili ya baadhi ya saratani Dkt. Maguha alisema saratani ya matiti huweza kujitokeza kwa uvimbe au mabadiliko katika titi. Kwa saratani ya mlango wa kizazi, dalili ni pamoja na kutokwa na damu ukeni bila mpangilio au wakati wa kujamiiana huku saratani ya tezi dume ikihusishwa na matatizo ya kukojoa au uvimbe.
“Saratani inaweza kuzuilika kwa kuepuka uvutaji wa sigara, kupunguza matumizi ya pombe, kula lishe bora, kufanya mazoezi, kupunguza uchafuzi wa mazingira na kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara. Ni muhimu kwa akina mama kunyonyesha Watoto na kujikinga na mionzi ya jua kwa watu wenye ualbino”, alisema Dkt. Maguha.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Juma Mkomi, Kaimu Katibu Mkuu ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uendelezaji Sera, Sailas Kapinga aliwashukuru wataalamu wa ORCI kwa kutoa elimu hiyo muhimu na kuwahimiza wafanyakazi kutumia fursa hiyo kupima afya zao ili kubaini mapema magonjwa na kuchukua hatua stahiki kabla hayajawa makubwa.
Kapinga alisisitiza kuwa uchunguzi wa mara kwa mara ni nguzo muhimu ya kinga na kuhimiza kila mtumishi kuweka afya yake kuwa kipaumbele kwa kujitokeza kupima bila kusubiri dalili kujitokeza.
Licha ya kutoa elimu kwa umma, wataalamu hao wa ORCI pia wanatoa ushauri wa kibingwa wa magonjwa ya saratani, huduma za vipimo mbalimbali vya saratani ikiwemo saratani ya tezi dume, ini, mlango wa kizazi, matiti na chanjo ya homa ya ini.