Latest Articles

CRDB BANK MKOANI MOROGORO YAFUTURISHA

 


Mwandishi wetu, Morogoro
MKUU wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima, amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani, umoja na mshikamano katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na hata baada ya kumalizika kwa mwezi huo.

RC Malima ametoa wito huo wakati akizungumza kwenye futari iliyoandaliwa na Benki ya CRDB kwa ajili ya wateja wake pamoja na wadau mbalimbali wa benki hiyo mkoani Morogoro.

Amesema kipindi cha Ramadhani ni muda muhimu kwa waumini wa Kiislamu kujitathmini, kufanya ibada na kuimarisha mahusiano mema, huku akisisitiza kuwa maombi yana mchango mkubwa katika kulinda amani na maendeleo ya taifa.

“Niwaombe Watanzania wote kutumia kipindi hiki cha Ramadhani kumuomba Mwenyezi Mungu alinde amani ya nchi yetu na atupe moyo wa upendo na mshikamano ili tuendelee kujenga taifa lenye maendeleo,” alisema Malima.

Aidha, alimshukuru Benki ya CRDB kwa kuandaa futari hiyo ambayo imewaleta pamoja viongozi, wateja na wadau mbalimbali katika kuimarisha mahusiano na mshikamano ndani ya jamii.

Kwa upande wake, Meneja wa Kanda ya Kati Benki ya CRDB Bi Chabu Mishwaro amesema lengo la kuandaa futari hiyo pamoja na dua maalum ni kushiriki ibada na kuungana na wateja wao katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.

Amesema benki hiyo imekuwa na utaratibu wa kukutana na wateja wake katika kipindi cha mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani ili kuimarisha na kuendeleza ushirikiano wa kibiashara pamoja na kushirikiana katika matendo ya kijamii yenye kuleta baraka kwa jamii.

“Futari hii ni sehemu ya kuonesha kuthamini wateja wetu ambao wamekuwa nguzo muhimu ya mafanikio ya benki yetu. Tunathamini sana mahusiano haya na tunaamini kuungana katika ibada na dua kunaimarisha mshikamano wetu,” alisema.

Naye Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa wa benki hiyo Mussa Kitambi amesema imekuwa ni utamaduni wa CRDB Bank kuandaa futari kwa ajili ya wateja wake kila mwaka katika mwezi wa Ramadhani.

Amesema mwezi mtukufu wa Ramadhani ni chuo cha malezi ya kiroho na nidhamu kwa waumini wa Kiislamu, huku swaumu ikiwa ni ibada inayowafanya watu wengi kuelekeza mioyo yao katika kumtii Mwenyezi Mungu, kufanya wema na kusaidia wenye uhitaji.

Aliongeza kuwa benki hiyo imekuwa ikiendelea kutoa huduma mbalimbali zinazozingatia mahitaji ya wateja Waislamu, ikiwemo programu maalum za huduma za kifedha zisizo na riba ili kuwawezesha kutimiza majukumu yao ya kiibada na kimaendeleo kwa mujibu wa misingi ya dini ya Kiislamu.

“Tunatoa huduma za uwezeshaji wa kifedha zisizo na riba kwa wateja wetu ili kuwasaidia kutekeleza shughuli zao za kiuchumi bila kwenda kinyume na misingi ya imani yao. Tunawaomba wateja wetu waendelee kuiamini na kushirikiana na benki yetu,” alisema.

Futari hiyo pia iliambatana na utoaji wa zawadi na misaada mbalimbali kwa watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu, ikiwa ni sehemu ya juhudi za benki hiyo kurejesha kwa jamii na kuonesha mshikamano katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.






read more

DKT AKWILAPO AKABIDHI VIFAA TIBA KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA MASASI

Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amekabidhi vifaa tiba katika Kituo cha Afya Mbonde kilichopo Halmashauri ya Mji Masasi mkoani Mtwara kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Dkt. Akwilapo amekabidhi vifaa hivyo leo, Machi 9, 2026, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma za afya katika Wilaya ya Masasi na maeneo jirani ya wilaya hiyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Dkt. Akwilapo amesema utoaji wa vifaa tiba ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha taasisi za huduma za jamii kama vile hospitali na shule zinakuwa na miundombinu na vifaa vinavyowawezesha wataalamu kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Amesema, serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha sekta za afya na elimu zinaimarika ili wananchi waweze kupata huduma bora karibu na maeneo yao.

“Naishukuru serikali chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha siyo tu inajenga majengo ya hospitali na shule, bali pia inahakikisha kunapatikana vifaa pamoja na wataalamu watakaowezesha huduma kutolewa kwa ufanisi,” amesema Dkt. Akwilapo.

Ameongeza kuwa, kupatikana kwa vifaa tiba katika Kituo cha Afya Mbonde, ikiwemo mashine maalum ya kusaidia watoto waliozaliwa kabla ya muda, kutasaidia kuokoa maisha ya watoto hao.

Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mbonde, Dkt. Mohamed Abbas, amesema, vifaa vilivyopokelewa vitasaidia kuimarisha huduma mbalimbali ikiwemo huduma kwa watoto, chumba cha upasuaji pamoja na huduma za maabara.

Kwa mujibu wa Dkt Abbas, kituo hicho cha afya Mbonde kinahudumia zaidi ya wananchi 32,000 kutoka kata tatu za Sululu, Mtawale na Mwenge Mtapika. Pia kituo kinatoa huduma kwa wagonjwa wanaotoka Halmashauri za Masasi na Nanyumbu.

Dkt. Abbas ameongeza kuwa, kituo hicho kinatoa huduma mbalimbali zikiwemo upasuaji, huduma za kulaza wagonjwa, uzazi pamoja na maabara.

Katika hatua nyingine, Mbunge huyo wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo pia amekabidhi vitabu 3,667 kwa shule 12 za Halmashauri ya Mji Masasi kwa lengo la kusaidia shughuli za ufundishaji na ujifunzaji.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vitabu hivyo Machi 9, 2026, mara baada ya kukutana na watendaji wa sekta ya elimu katika halmashauri hiyo, Dkt. Akwilapo amesema vitabu ni nyenzo muhimu katika kuboresha elimu shuleni.

“Kama tunavyojua, ufundishaji unahitaji zana, na moja ya zana muhimu ni vitabu. Hii ni awamu ya kwanza ya msaada huu na tutakuja tena na awamu ya pili, lengo ni kuwapa walimu nafasi ya kufanya kazi kwa ufanisi zaidi,” amesema.

Amesema, hatua hiyo inalenga kuimarisha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji ili kuongeza ubora wa elimu kwa wanafunzi wa shule hizo.

Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi moja ya vifaa tiba Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mbonde kilichopo Masasi mkoani Mtwara Dkt Mohamed Abbas wakati wa ziara yake mkoani humo.


Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akipata maelezo ya moja ya kifaa tiba kutoka kwa Mganga Mfawadhi wa Kituo cha Afya Mbonde Dkt Mohamed Abbas wakati wa ziara ya Jimbo tarehe 9 Machi 2026.

Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo pamoja na viongozi wengine wakiwa katika picha na moja ya vifaa tiba alivyokabidhi katika hospitali ya Mbonde Masasi tarehe 9 Machi 2026.


Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akisalimiana na mmoja wa wagonjwa waliokwenda kupata huduma katika Kituo cha Afya Mbonde Masasi mkoani Mtwara tarehe 9 Machi 2026.


Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi vitabu mmoja wa walimu wa shule za sekondari katika halmashauri ya Mji Masasi alipotoa vitabu 3,667 kwa sekondari za halmashauri hiyo tarehe 9 Machi 2026.


Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akionesha moja ya vitabu alivyokabidhi kwa shule za sekondari mara baada ya kuvikabidhi tarehe 9 Machi 2026.

Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa sekta ya elimu katika halmashauri ya Mji Masasi mara baada ya kukabidhi vitabu 3,667 kwa shule za sekondari tarehe 9 Machi 2026.
read more