Latest Articles

JKT YAREJEA WITO KWA VIJANA WALIOCHELEWA KURIPOTI MAKAMBINI, WARUHUSIWA KURIPOTI HADI JUNI 15, 2026

 Na Mwandishi wetu Michuzi TV


Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limetoa nafasi ya mwisho kwa vijana waliohitimu elimu ya sekondari ngazi ya Kidato cha Sita mwaka 2026 na kuchaguliwa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria, lakini bado hawajaripoti katika makambi waliyopangiwa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Juni 12, 2026, jijini Dodoma na Makao Makuu ya JKT, vijana hao wametakiwa kuripoti kuanzia leo hadi Juni 15, 2026 ili kuendelea na mafunzo yao.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Tawi la Operesheni na Mafunzo JKT, Peter Mnyani, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, Rajabu Nduku Mabele.

JKT imeeleza kuwa vijana ambao hawakufanikiwa kufika katika makambi waliyoelekezwa awali wanapaswa kuripoti katika kambi za JKT zilizo karibu na maeneo wanayoishi ili kurahisisha usajili na kuendelea na mafunzo.

Hata hivyo, Jeshi hilo limefafanua kuwa utaratibu huo hauhusishi vijana wanaotakiwa kuripoti katika Kambi ya Makutupora JKT Camp, Kambi ya Ruvu JKT Camp pamoja na Kambi ya Chuo cha Uongozi Kimbiji, ambazo hazijajumuishwa katika mwongozo huo wa kuripoti kwenye kambi zilizo karibu.

JKT imewasisitiza vijana wote husika kutumia fursa hiyo ya nyongeza ya muda kuhakikisha wanaripoti ndani ya kipindi kilichotolewa ili kutimiza wajibu wao wa kujiunga na mafunzo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.

read more

KIKWETE AKUTANA NA MSHARI WA TRUMP PEMBEZONI MWA MKUTANO WA OSLO FORUM

  


Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Massad Boulos, mwanadiplomasia na Mshauri Mwandamizi wa Rais Donald Trump kuhusu masuala ya Afrika, nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati, baada ya kufanya mazungumzo pembezoni mwa Mkutano wa Oslo Forum unaofanyika Oslo, Norway.


Mkutano huo, unaofanyika kuanzia tarehe 10 hadi 12 Juni, 2026, umewakutanisha viongozi, wanadiplomasia waandamizi na wadau wa masuala ya amani, diplomasia na usuluhishi kutoka nchi mbalimbali zenye ushawishi duniani.
read more

WAGONJWA NANE WENYE MISHIPA YA DAMU ILIYOZIBA KUFANYIWA UPASUAJI WA MOYO

 

Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na mwenzao kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India Upendra Bhalerao kumfanyia upasuaji wa kupandikiza mshipa wa damu wa moyo bila kusimamisha moyo mgonjwa mwenye matatizo ya mishipa ya damu kuziba wakati wa kambi maalumu ya siku nane inayofanyika katika Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.

Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo, mishipa ya damu na kifua kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India Upendra Bhalerao akitoa mafunzo kwa wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) namna ya kutoa huduma kwa wagonjwa ambao mshipa yao ya damu imeziba wakati wa kambi maalumu ya siku nane inayofanyika katika Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.


Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo, mishipa ya damu na kifua kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India Upendra Bhalerao akiangalia taarifa za mgonjwa aliyelazwa katika wodi ya uangalizi maalumu (ICU) mara baada ya kufanyiwa upasuaji wa kupandikiza mshipa wa damu wa moyo bila kusimamisha moyo wakati wa kambi maalumu ya siku nane inayofanyika katika Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.
***************************************************************************************************
Wagonjwa nane wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba (coronary artery disease) kufanyiwa upasuaji wa kupandikiza mishipa ya damu ya moyo bila kusimamisha moyo (off Pump CABG).

Upasuaji huo unafanyika katika kambi maalumu ya siku nane inayofanywa na watalaamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii leo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba watumie kambi hiyo kupata matibabu na kupunguza gharama ambazo wangetumia kusafiri nje ya nchi kwaajili ya matibabu.

“Upasuaji huu unafaida kubwa kwa wagonjwa ambao wamekuwa wakitumia dawa kwa muda mrefu kwa kupata matibabu kwani unafanyika bila kusimamisha moyo na unamsaidia mgonjwa kupona kwa muda mfupi na kuendelea na shughuli zake za kawaida”, alisema Dkt. Angela.

Dkt. Angela alibainisha kuwa kupitia kambi hiyo wataalumu wa JKCI watapata fursa ya kujengewa uwezo na kubadilishana uzoefu na wenzao kutoka India jambo mbalo litasaidia kuimarisha zaidi huduma za upasuaji na mishipa ya moyo nchini.

“Tayari tumemfanyia upasuaji mgonjwa mmoja ambaye mishipa mitatu ya moyo ilikuwa imeziba kwa mafanikio makubwa na tunatarajia kuwafanyia upasuaji wagonjwa nane katika kambi hii”, alisema Dkt. Angela.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo na Mishipa ya Damu kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India Upendra Bhalerao alisema upasuaji huo unafanyika kwa ufanisi mkubwa kutokana na uwekezaji mkubwa wa vifaa tiba uliofanywa na Serikali ya Tanzania kupitia JKCI.

“Tumekuwa tukija Tanzania mara kwa mara kutokana na ushirikiano mzuri wa kitabibu uliopo kati ya India na Tanzania na kuwasaidia wagonjwa ambao wanatumia gharama kubwa kufuata matibabu India hivyo uwepo wetu hapa umekuwa ukiwapunguzia adha wagonjwa wenye matatizo ya mishipa yad amu ya moyo iliyoziba”, alisema Bhalerao.

Kambi hiyo maamulu ya upasuaji wa mishipa ya damu ya moyo iliyoziba inatarajiwa kumalizika mapema tarehe 15 mwezi Juni mwaka huu.

read more

RAIS WA SHIRIKA LA KIMATAIFA LA MADAKTARI WA AFYA YA KINYWA NA MENO DUNIANI (FDI) DR. NIKOLAI SHARKOV ATEMBELEA MABANDA MAONESHO YA PILI YA BIDHAA ZA KINYWA NA MENO ZA KIMATAIFA (DENTAL EXPO)

 

Rais wa Shirika la Kimataifa la madaktari wa Afya ya Kinywa  na Meno Duniani (FDI) Prof. Dr. Nikolai sharkov akizungumza na washiriki wakati wa Maonesho ya Pili ya Bidhaa za Kinywa na Meno za Kimataifa (Dental EXPO) leo Mei 28 Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam ambayo yanatarajiwa kumalizika Mei 30,2026.

Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Edna Kajuna akizungumza na Rais wa Shirika la Kimataifa la madaktari wa Afya ya Kinywa na Meno Duniani (FDI) Prof. Dr. Nikolai sharkov alipotembelea Banda la Taasisi hiyo katika Ukumbi wa Mlimani City wakati wa Maonesho ya Pili ya Bidhaa za Kinywa na Meno za Kimataifa (Dental EXPO) leo Mei 28 Dar es Salaam ambayo yanatarajiwa kumalizika Mei 30,2026.

Washiriki wakimsikiliza Rais wa Shirika la Kimataifa la madaktari wa Afya ya Kinywa  na Meno Duniani (FDI) Prof. Dr. Nikolai sharkov alipokuwa akizungumza wakati wa Maonesho ya Pili ya Bidhaa za Kinywa na Meno za Kimataifa ( Dental EXPO) leo Mei 28 Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam ambayo yanatarajiwa kumalizika Mei 30,2026.

Wasanii wa Kikundi cha Kusa Bendi wakinogesha Maonesho ya Pili ya Bidhaa za Kinywa na Meno za Kimataifa (Dental EXPO) leo Mei 28 katika Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam ambayo yanatarajiwa kumalizika Mei 30,2026.

read more

TDA NA SHIRIKISHO LA AFYA YA KINYWA NA MENO DUNIANI (FDI) WAAHIDI KUENDELEZA USHIRIKIANO NA MUHAS

 Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania (TDA) na Shirikisho la Madaktari wa Meno Duniani (FDI) wameahidi kuendeleza uhsirikiano na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) katika kuendeleza elimu ya tiba ya meno na huduma za afya.


Ahadi ya ushirikiano huo ilifikiwa mwishoni mwa wiki, wakati Mkuu wa Shule Kuu ya Afya ya Kinywa na Meno, Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) Dkt. Ferdinand Machibya, alipokuwa akizungumza na Rais wa Shirikisho la kinywa na Meno Duniani (FDI), Prof. Nikolai Sharkov, ambaye alitembelea MUHAS akiwa na ujumbe wake kutoka FDI kwa lengo la kuongeza ushirikiano kati ya MUHAS na washirika wa kimataifa katika kuendeleza elimu ya tiba ya meno na huduma za afya.

Ziara hiyo iliwakutanisha wataalamu wa tiba ya meno, wahadhiri, pamoja na wanafunzi kwa ajili ya kujadili fursa za ushirikiano katika mafunzo, utafiti, na kujengeana uwezo ndani ya sekta ya afya ya meno.

Akizungumza wakati wa mkutano huo, Dk. Machibya, alimkaribisha, Prof. Nikolai Sharkov, chuoni hapo. Alieleza kuwa ziara hiyo inaonesha kuongezeka kwa ushirikiano kati ya MUHAS na washirika wa kimataifa katika kuendeleza elimu ya tiba ya meno na huduma za afya.

Dk. Machibya alisema MUHAS inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika kuzalisha wataalamu wenye ujuzi kupitia ufundishaji, utafiti, pamoja na huduma za ushauri wa kitaalamu. Aliongeza kuwa Shule ya Tiba ya Meno imekuwa ikivutia wanafunzi wa shahada za uzamili na wataalamu kutoka nchi mbalimbali wanaojiunga na chuo hicho kwa ajili ya mafunzo maalum na kozi fupi za afya.

Katika ziara hiyo, Prof. Sharkov aliipongeza Shule ya Tiba ya Meno ya MUHAS kwa mchango wake katika sayansi ya afya ya kinywa na meno, na kuisifu shule hiyo kwa kuwa Kituo Bora cha Umahiri katika Sayansi ya Afya ya Kinywa na Meno Afrika Mashariki.

Kwa upande wake, Prof. Sharkov pia aliipongeza MUHAS pamoja na Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania kwa mchango wao katika kuimarisha huduma za afya ya meno na kuzalisha wataalamu wenye sifa nchini Tanzania.

Aidha, aliwahimiza wanafunzi wa tiba ya meno kuendelea kuwa makini katika masomo yao na kukuza taaluma zao ili waweze kuchangia ipasavyo katika mustakabali wa huduma za afya ya kinywa na meno.

Tukio hilo lilifanyika katika Shule ya Tiba ya Meno MUHAS na kuhudhuriwa na viongozi wa Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania, madaktari wa meno wa kanda mbalimbali, wahadhiri wa MUHAS, pamoja na wanafunzi. 

read more

RAIS WA TDA DK. BEREGE ASEMA UJIO WA RAIS WA FDI PROF. SHARKOV UMEWAONGEZEA CHACHU WANATAALUMA, AFYA YA KINYWA NA MENO

Na Khamis Mussa, Muhimbili
Rais wa Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania (TDA) Dk. Gemma Berege, amesema ujio wa Rais wa Shirikisho la Madaktari wa Meno Duniani (FDI), Prof. Nikolai Sharkov umewaongezea chachu wao kama wanataaluma  na kuwafanya kudumu na kudumu zaidi katika misingi ya majukumu yao ya kila siku.


Amesema, ujio huo unawaongezea chachu kwa kuwa umegusa jukumu lao kubwa ambalo ni kulinda taaluma yao ikiwemo kwa kujiongeza katika elimu. "Tumefurahi kwamba hata katika mazungumzo yake Prof Sharkov, amesisitiza ushirkiano na kujituma, hivyo ametuongezea ari", alisema Dk. Berege.

Dk. Berege alisema pia ujio wa Prof Sharkov umeleta ari kwa vyama vya wanafunzi ambao kwa kuwa wamekuwa wakikutana naye kupitia wawakilishi wao na kupata ya kujifunza mengi kupitia kwake (Prof, Sharkov).

Kwa upande wake Prof, Sharkov ambaye alikuwa nchini na kupata fursa ya kukutana na viongozi wa TDA na Shule ya Tiba ya Meno ya MUHAS, aliwapongeza kwa mchango wao katika kuimarisha huduma za afya ya meno na kuzalisha wataalamu wenye sifa nchini Tanzania.

Pia amewahimiza wanafunzi wa tiba ya meno kuendelea kuwa makini katika masomo yao na kukuza taaluma zao ili waweze kuchangia ipasavyo katika mustakabali wa huduma za afya ya kinywa na meno.

Prof. Sharkov, alikutana na viongozi hao Mei 29, 2026, ambapo akiambatana na ujumbe wa TDA alitembelea MUHAS katika juhudi za kuimarisha ushirikiano katika elimu ya tiba ya meno na maendeleo ya taaluma hiyo.

Nyakati za mazungumzo na Prof. Sharkov, walihudhuria viongozi hao wa TDA, madaktari wa meno wa kada mbalimbali, wahadhiri wa MUHAS na wanafunzi kwa ajili ya kujadili fursa za ushirikiano katika mafunzo, utafiti, na kujengeana uwezo ndani ya sekta ya afya ya meno.

Dk. Berege akimpatia zawadi ya picha Prof Sharkov alipofika ofisi ya TDA.

Dk. Berege akimpatia zawadi ya fulana Prof Sharkov alipofika ofisi ya TDA.

Dk. Berege akimpatia maelezo kwa Prof Sharkov. kuhusu beji ya TDA kabla ya kumkabidhi.

read more

MBUNGE KIGOMA MJINI CLAYTON CHIPANDO ATAKA KITENGO CHA ELIMULISHE

 
   Mbunge wa Kigoma Mjini, Clayton Chipando, (Baba Levo) akichangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 leo jijini Dodoma
 
**************************************************************************************************************************
Mbunge wa Kigoma Mjini, Clayton Chipando, (Baba Levo) ameshauri Wizara ya Afya kuwa na Kitengo maalum kwa ajili ya kutoa elimu Afya ya Lishe Mitandaoni dhidi ya baadhi ya watu wanaotoa Elimu hiyo bila kuwa na mwongozo sahihi wa Wizara yenye dhamana ya Afya.
 
Mhe. Chipando ameyasema hayo Mei 12, 2026 jijini Dodoma wakati akichangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 
 
"Mhe. Mwenyekiti mimi nimekula Ugali kwa miaka 35, lakini Leo kila ukiingia mtandaoni utakutana na matangazo mbalimbali yanayotumika kuelimisha watu juu ya utaratibu wa matumizi ya chakula" amesema Mhe. Chipando
 
Mhe. Chipando amesema katìka siku za hivi karibuni kumekuwepo na wimbi la watoa huduma, ambao kwa namna moja au nyingine wamekuwa wakitoa elimu kuhusu lishe na kuwaweka wananchi kwenye mtanziko wa nini wale na kiwango gani.
 
Kwa upande wake Mhe. Khamis Ali Vuai Mbunge wa Jimbo la Mkwajuni (CCM) mkoani Kaskazini UngujaMbunge  aliyeomba kutoa taarifa wakati wa Mchango huo, aliliambia Bunge  kuwa taifa la India ni moja ya Taifa lililoweka Utaratibu wa nani atatoa elimu ya Afya, hivyo kama Taifa tuone kama kitu muhimu, jambo lililokubaliwa na Mchangiaji.
 
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeendelea na Uchangiaji wa Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52,  kwa mwaka wa fedha 2026/27 iliyowasilishwa Mei 11, 2026 Bungeni na Waziri wa Afya Mhe Mohamed Mchengerwa na kuomba kuidhinishiwa kiasi cha shilingi Trilioni 1.8 kwa ajili yakutekeleza vipaumbele 11.M
read more