WASHTAKIWA NANE WAKIWEMO ASKARI WAWILI JWTZ WANAODAIWA KUKUTWA NA KOBE 116 BILA VIBALI WASOMEWA MASHARTI YA DHAMANA

 MAHAKAMA  ya Hakimu Mkazi Kisutu imewasomea masharti ya dhamana washtakiwa nane wakiwemo mwanajeshi kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), wanaodaiwa kukutwa na nyara za serikali ambazo ni Kobe 116 bila ya kuwa na kibali.



Hata hivyo, washtakiwa katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi, wamesomewa masharti ya dhamana bila ya wao kuwepo mahakamani kutokana na changamoto za usafiri kutoka gerezani.

Akisoma masharti hayo Hakimu Mkazi Mkuu,  Rhoda Ngimilanga amewataka washtakiwa kila mmoja kuwa na wadhamini wawili wanaoishi Dar es Salaam, wenye barua na vitambulisho vya Nida na watakaosaini bondi ya sh. Milioni tano. 


Washtakiwa katika kesi hiyo ni, mfanyabiashara Josephat Moyo (52) mkazi wa Tabata, Deogratius Lugeng'a (40),  MT 88046 Sajenti Cosmas Ndomba kutoka JWTZ na  Mfanyabiashara Hamza Abdalah ( (52).


Wengine ni MT 118102 Kassim Abdalah (35), Nkanamuli Ngaza (52)  mlinzi kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere na wakukima wawili Kutoka mkoa wa Dodoma ambao ni  Stephano Chedego (51) na Mwaluko Mgomole.


 Wote kwa pamoja wanakabiliwa na kesi ya uhujumu Uchumi yenye mashitaka matatu likiwemo la kuongoza genge la uhalifu na kujihusisha na nyara za serikali ambazo ni kobe 116 bila kibali.


Inadaiwa, kati ya Januari mwaka hadi Julai 3 mwaka 2022 ,Dar es Salaam, washtakiwa hao waliendesha genge la uhalifu kwa kununua, kukusanya, kusafirisha, na kuuza nyara za Serikali ambazo ni Kobe 116  wenye thamani ya USD  8120 sawa na sh
 18,935,840.


Katika shitaka la pili imedaiwa, katika tarehe isiyojulikana mkoani  Dar es Salaam, washtakiwa  kwa pamoja walijihusisha na nyara hizo za serikali kwa kununua na kuziuza bila kuwa na kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori.


Pia,  Julai 3 mwaka 2022 katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, washitakiwa hao walikutwa na kobe hao bila kuwa na kibali.


Kesi hiyo imeahirishwa hadi Januari 30, 2023 washtakiwa watakapoletwa mahakamani kwa ajali ya kuangalia kama upelelezi umekamilika na kudhaminiwa iwapo watakuwa wametimiza masharti ya dhamana.

0 comments: