Wakati habari na ripoti mbalimbali zinaeleza
kuwa makundi ya kigaidi yanakaribia kushindwa kikamilifu katika eneo la
mashariki mwa mji wa Aleppo nchini Syria, Marekani inafanya jitihada
kubwa za kuhakikisha inazuia ushindi wa jeshi la Syria dhidi ya magaidi
hao.
Jeshi la Syria likisaidiwa na ndege za kijeshi za Russia na
washauri wa kijeshi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran linakaribia kupata
ushindi mkubwa huko Aleppo ambayo imekuwa miongoni mwa ngome kuu za
makundi ya kigaidi nchini Syria kwa kipindi cha zaidi miaka 5 sasa.
Kukombolewa eneo la mashariki mwa Aleppo hautakuwa mwisho wa uhai wa
makundi ya kigaidi nchini Syria lakini ni hatua kubwa katika uwanja huo.
Kwa msingi huo wasaidizi na waungaji mkono wa makundi hayo ya kigaidi,
hususan Marekani na Saudi Arabia, katika siku za hivi karibuni wanafanya
jitihada kubwa za kuishawishi Russia ikubaliane na usitishaji vita
nchini Syia. Kama ilivyokuwa huko nyuma ambapo Marekani ilikuwa ikitumia
kisingizio cha kutokea maafa ya kibinadamu na kutoa wito wa kusitishwa
vita wakati inapoona magaidi wanakaribia kuangamizwa, mara hii pia
Washington inataka kutumia kisingizio na mbinu hiyo hiyo.
Jeshi la Syria linaendelea kupata ushindi Aleppo
Pamoja na hayo na licha ya serikali ya Russia kukubali wazo la
kufanyika mazungumzo mapya ya kusimamisha vita huko Aleppo, lakini
Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia Sergei Lavrov amesisitiza kuwa,
Washington imechukua misimamo ya kustaajabisha na inayogongana kuhusu
suala la kuwaruhusu raia kuondoka kwenye medani ya mapigano katika eneo
hilo.
Misimamo hiyo ya kustaajabisha na ya kukinzana ya Marekani ni
kielelezo kwamba, Washington umekiri kwa njia isiyo ya moja kwa moja
kwamba eneo la mashariki mwa Aleppo limekombolewa kutoka kwenye makucha
ya makundi ya kigaidi. Kwa utaratibu huo, Marekani inatoa wito wa
kusitishwa mashambulizi ya jeshi la Syria na waitifaki wake huko Aleppo
kwa shabaha ya kuokoa si maisha ya raia wa kawaida wa Syria bali magaidi
wanaohaha wakikimbia huku na kule na hatimaye kuzuia kushindwa
kikamilifu makundi hayo katika siku za mwishoni mwa uongozi wa Rais
Barack Obama.
Rais Barack Obama wa Marekani
Kufeli kwa mazungumzo ya awali kati ya Marekani na Russia juu ya vita
nchini Syria ambako ni matokeo ya siasa zinazogongana na serikali ya
Washington, kumelifanya jeshi la Syria lizidishe juhudi za kulikomboa
eneo la mashariki mwa Aleppo na sasa ni robo tu ya mashariki mwa eneo
hilo ndiyo iliyobakia katika makucha ya magaidi hao wanaoungwa mkono na
Marekani, Israel, Saudi Arabia na washirika wao.
Licha ya kukabiliana na changamoto mbili kubwa katika vita vya
Aleppo, yaani changamoto ya hali ya raia wa kawaida kutokana na idadi
yao kubwa na msongamano wa nyumba na vilevile hatua ya makundi ya
upinzani na kigaidi ya kukataa kusalimu amri, lakini jeshi la Syria
linaendeleza operesheni hiyo kwa tadbiri ya hali ya juu na umakini
mkubwa.
Idadi kubwa ya raia na msongamano wa nyumba, tatizo kuu katika vita vya Aleppo
Hapana shaka kuwa katika siku zijazo pia Marekani itaendelezajuhudi
za kutaka kuzuia ushindi kamili na mkubwa wa jeshi la Syria huko Aleppo.
Katika uwanja huo ripoti zinasema kuwa, Rais Barack Obama wa Marekani
ameondoa baadhi ya vizuizi vya kuwatumia silaha za kisasa waasi na
magaidi katika vita vya kukomboa mji wa Raqqah. Kwa hatua hiyo ya Obama,
sasa Marekani inaweza kutoa silaha zaidi kwa makundi ya waasi ambayo
yako tayari kushiriki katika vita dhidi ya serikali ya Syria katika mji
wa Raqqah
0 comments: