KUENEA MAGONJWA YA KUAMBUKIZA YEMEN SAMBAMBA NA JINAI ZA WASAUDIA
Posted by khamisimussa77@gmail.com at 12:11 PM
Katika hali ambayo kuenea kwa magonjwa ya
kuambukiza kama vile kipindupindu nchini Yemen kumepelekea makumi ya
watu kupoteza maisha, makumi ya raia wengine wa nchi hiyo wanaendelea
kupoteza maisha kutokana na hujuma za ndege za kivita za Saudia.
Ikitangaza habari hiyo hapo jana Alkhamisi Disemba 8, Wizara ya
Afya ya Yemen imesema kuwa magonjwa ya kuambukiza yameenea katika mikoa
15 ya nchi hiyo na kusababisha vifo vya watu 89. Wakati huo huo jana
ndege za kivita za Saudia na washirika wake ziliendeleza hujuma za
kichokozi katika mji wa Sanhan na eneo la Bahlul katika mkoa wa San'aa
na vilevile katika mkoa wa Saada na kusababisha maafa, majeraha na
hasara kubwa katika maeneo hayo. Mbali na maafa ambayo yamesababishwa na
hujuma hiyo ya kinyama ya Saudia ambayo imeingia katika mwezi wa 21
tokea ianzishwe, wananchi wa Yemen pia wamekuwa wahanga wa magonjwa ya
kuambukiza ambayo yameenea nchini humo kutokana na huduma duni za afya
kutokana na kuharibiwa miundombinu muhimu ya nchi hiyo, ikiwemo ya afya
katika uchokozi huo wa Saudia na washirika wake.
Hujuma hiyo ya kijeshi imepelekea kuharibiwa asilimia 80 ya
miundombinu hiyo muhimu katika maeneo ya mijini na hasa vituo vya afya
na tiba. Mwezi Agosti mwaka huu, Shirika la Afya Duniani WHO lilitangaza
kuwa ni asilimia 45 tu ya vituo vya afya vya Yemen ndivyo vinavyofanya
kazi ikiwemo asilimia 37 pekee ya hospitali za nchi hiyo. Uhaba wa maji
na chakula ni sababu nyingine ya kuenea magonjwa hayo ya kuambukiza,
tatizo ambalo limekuwa kubwa zaidi kufuatia hujuma ya ndege za Saudia.
Hali hiyo bila shaka imezidisha vifo vinavyotokana na magonjwa ya
kuambukiza. Kuhusiana na suala hilo, katika ripoti yake ya hivi
karibuni, Abdul Hakim al-Kahlani, mkuu wa kitengo cha kupambana na
magonjwa ya kuambukiza katika Wizara ya Afya ya Yemen ametangaza kuwa
watu 11 wamepoteza maisha yao kutokana na kipindupindu na wengine 78
kutokana na magonjwa ya utumbo au mfumo wa mmeng'enyo wa chakula.
Abdul Hakim al-Kahlani anaendelea kusema kuwa hivi sasa amepokea kesi
za watu 138 wengine ambao wameathirika na kipindupindu katika mikoa 15
ya Yemen. Siku kadhaa zilizopita Shirika la Afya Duniani WHO
lilitahadharisha kuhusiana na hatari ya kuenea kipindupindu nchini Yemen
na kutangaza kuwa ugonjwa huo tayari umeathiri nusu ya mikoa ya nchi
hiyo. Kwa kuzingatia hali hiyo ya kutisha, ndege za kivita za Saudia
bado zinashambulia maeneo tofauti ya nchi hiyo. Kufikia sasa zaidi ya
Wayemen 10,000 wamepoteza maisha yao moja kwa moja kutokana na
mashambulio hayo ya kinyama. Jambo la kushangaza ni kuwa nchi za
Magharibi ambazo zinapiga makelele na kusisitiza juu ya kusitishwa vita
huko Halab nchini Syria ili kuwapa mwanya wa kupumua magaidi wanaotenda
jinai na ukatili dhidi ya raia wa nchi hiyo, wamekaa kimya na kutofanya
juhudi zozote za kusitisha hujuma ya Saudia nchini Yemen ili kuokoa
maisha ya raia wasio na hatia wa nchi hiyo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: