SERIKALI IPUNGUZE USHURU WA MAZAO YA MISITU

NA MAGRETH MAGOSSO,KIGOMA

SERIKALI imeshauriwa iangalie upya viwango vya utozaji wa ushuru katika rasilimali za umma,ili kuondoa urasimu unaofanywa  na baadhi ya watumishi wa umma  kwa nia ya kuidhofisha  serikali ya awamu ya Tano  yenye dhati ya kupunguza umaskini wa kipato kwa walalahoi.

Ushauri huo umetolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Wauza mkaa mkoani kigoma   Fadhili Hamisi wakati akizungumza na Gazeti hili juzi katika kijiji cha Mazungwe kilichopo Halmashauri ya wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma.

Alisema changamoto iliyopo katika rasilimali za umma hasa zao la misitu katika uvunaji wa bidhaa ya mkaa imekuwa ya utata kwa walio na kibali cha uvunaji wa zao hilo,ambapo idara ya misitu ina hulka ya kutoa kibali kwa wadau lakini haielekezi eneo la uvunaji.

Alifafanua kuwa,kitendo cha kutoa kibali bila eneo elekezi inachangia wenye vibali kuvamia kila pori analodhani ni fursa kwake kwa lengo la kufanya biashara kwa mujibu wa kibali chake,hali inayotishia  janga la njaa siku zijazo kwa kuwa,miti inakatwa holela kitendo kinachochangia mabadiliko ya tabia Nchi.

Hamisi alishauri serikali ipunguze  ushuru usio na tija ya kuokoa rasilimali misitu,akitolea mfano wa gunia moja la mkaa lenye ujazo wa kilo 100 linalipiwa kwa kiasi cha fedha sh.27,500 ambapo serikali kuu inachukua sh.240 kwa kila kilo ya mkaa na sh.1,000 kwa ajili ya upandaji miti .

Alisema kitendo hicho kinachangia  rushwa na urasimu baina ya watumishi wa idara husika na wavunaji ambao  wanafanya biashara kwa mujibu wa mazingira wanayowekewa na kwa ushuru wa sh.27,500  wanapaswa wauze gunia moja la mkaa kwa sh.60,000 hali ambayo ingeathiri uchumi wa wajasiliamali wengi hasa wapika vitafuno na walalahoikushindwa kumudu bidhaa.

Hamisi alitolea mfano wilaya ya uvinza ambayo inakabiliwa na urasimu wa ulipaji wa gharama za mkaa hata ukiwa na gunia moja ukalipie katika benki husika ambayo ipo wilaya ya kigoma mjini kisha urudishe stakabadhi katika halmashauri ya uvinza bila kujali athari ya gharama za uvunaji wa zao hilo ni uwepo wa rushwa.

Ameiomba serikali kupitia idara hiyo iondoe ushuru wa sh.240 kwa kilo moja ya mkaa hadi sh.150  kwa kila kilo moja ya mkaa ili wavunaji wenye kibali wavune zao hilo kwa sheria,taratibu zenye mashiko kwa wafanyabiashara wa mkaa ambao unatumika kwa wakubwa na wasio na kipato kikubwa.

Alipohojiwa Mkuu wa Wilaya ya Uvinza Mwanamvua Hoza juu ya kero  hiyo alisema ili kuondoa urasimu huo,walengwa wafikishe malalamiko kwa mandishi ofisnini kwake ili wayafanyie kazi kwa pamoja kwa lengo la kuondoa makandokando yasiyo na tija, ili kuimarisha uwajibikaji wa serikali ya awamu ya tano.
Mwisho.

0 comments: