Hayo yamesemwa leo jijini Dar es salaam na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt. Shukuru Kawambwa wakati akifungua warsha ya uwasilishaji wa ripoti ya upimaji wa kitaifa wa Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu maarufu KKK kwa darasa la pili uliofanyika mwezi Oktoba 2013.
Hata hivyo Waziri Dkt Kawambwa amesema matokeo ya utafiti uliofanywa na Shirika lisilo la Kiserikali la UWEZO mwaka 2010 yanaonesha kwamba zaidi ya asilimia 70 ya wanafunzi katika madarasa ya chini hawazimudu stadi za Kuandika, Kusoma na Kuhesabu kwa kiwango kinachotakiwa.
"Ni hakika kwamba, ufundishaji wa stadi za Kuandika, Kuhesabu na Kusoma unatakiwa ufanyike kwa makini hata hivyo upo ushahidi kwamba ufundishaji huo haufanyiki kama ilivyotarajiwa."Alisema Dkt Kawambwa
Amesema hali hiyo ya ufundishaji hafifu inajidhihirisha zaidi kwa matokeo ya ufaulu wa chini katika madarasa ya juu darasa la nne la saba.
Waziri Dkt Kawambwa amesema Ili kutatua changamoto hiyo na kuwezesha kuinua kiwango cha ubora wa elimu itolewayo,, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa kiushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) imeanza kutekeleza mkakati wa Matokeo Makubwa Sasa, (Big Results Now )
Amesema chini ya utekelezaji wa Makkati wa Matokeo Makubwa sasa katika sekta ya elimu upimaji wa kitaifa wa stadi za KKK na mafunzo kazini kwa walimu wa darasa la I & II kuhusu ufundishaji mahiri wa stadi hizo ni miongoni mwa mikakati 9 iliyoibuliwa.
Aidha Waziri huyo wa Elimu nchini ameishukuru serikali ya Marekani ambayo kupitia shirika la USAID, imewezesha kufanya upimaji wa kitaifa wa stadi za KKK ulioongozwa na taasisi ya "Research Triangle Institute"(RTI).
"Ni matarajio yangu kwamba matokeo ya upimaji huu uliofanyika kwa kutumia Zana za "Early Grade Reading Assessment (EGRA)", the "Early Grade Mathematics Assessment (EGMA)" na "Snapshot of School Management Effectiveness (SSME)" utaisaidia serikali kupata taarifa kuhusu hali halisi ya kumudu stadi za KKK kwa wanafunzi wa Darasa la Pili."Alisema
"Matokeo ya utafiti huu pia yatasaidia katika kulinganisha na matokeo ya upimaji wa darasa la pili unaotarajiwa kufanyika mwaka 2014 na 2015 pamoja na kusaidia serikali katika kuandaa programmu mbalimbali ili kufikia malengo tarajiwa ya kuinua ubora wa elimu na ufaulu"Aliongeza
.
Ushiriki wa Jamii na Wazazi katika masuala ya elimu ni muhimu ili kuinua upatikanaji wa elimu bora, upatikanaji wa rasilimali na kuongeza uwajibikaji.
Tanzania ina rekodi nzuri ya ushirikishaji wa jamii kupitia kamati za shule na taasisi za kiraia na hivyo Waziri Dkt Kawambwa ametumia fursa hiyo kutoa rai kwa wadau mbalimbali wa elimu kuwasaidia watoto kwa kuwawezesha kupata na kutumia stadi mbalimbali za lugha kupitia usomaji wa vitabu na kuzungumza nao wakiwa nyumbani ili hatimaye kuwawezesha kufanya vizuri wakiwa shule.
0 comments: