Thursday, November 24, 2016

KUENDELEA UKANDAMIZAJI DHIDI YA WAPINZANI NCHINI BAHRAIN NA WASIWASI WA IMATAIFA

Ripoti mbalimbali kutoka nchini Bahrain zinaonyesha kuwa, utawala wa kifalme wa nchi hiyo umeendelea kutumia mbinu na miamala yake ya kipolisi dhidi ya wanaharakti wa kisiasa huku ukiendelea kuwatia mbaroni na kuwahukumu vifungo vya muda mrefu jela wapinzani hao kwa kuwabambikiza tuhuma mbalimbali.
Katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita, makumi ya wanaharakati wa Bahrain wametiwa mbaroni. Aidha Jumatano ya jana mahakama moja ya nchi hiyo iliwahukumu kifungo cha maisha jela wanaharakati sita wa nchi hiyo, hatua ambazo zinabainisha kuendelea vitendo vya ukandamizaji dhidi ya wananchi wa nchi hiyo.
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Bahrain alidai Jumatano ya jana kwamba, wanaharakati hao sita ambapo wawili kati yao hawakuweko mahakamani wakati wa kutolewa hukumu hiyo, wamepatwa na hatia ya kupigana na vikosi vya usalama mjini Manama mwaka jana. Wakati huo huo, baada ya Nabil Rajab, Mkuu wa Kamati ya Haki za Binadamu ya Bahrain kushikiliwa kwa miezi mitatu katika chumba ya peke yake, Jumatano ya jana alipelekwa hospitali kutokana na matatizo ya moyo yanayomkabili.
Maandamano ya wananchi wa Bahrain
Jinai za utawala wa kifalme wa Aal Khalifa nchini Bahrain dhidi ya wananchi wa nchi hiyo zinaendelea kushuhudiwa katika hali ambayo, Shirika la Msamaha Duniani la Amnesty International limetangaza kuwa, muamala mbaya dhidi ya wafungwa ikiwemo vitendo vya mateso dhidi ya wafungwa hao vingali vinaendelea kushuhudiwa katika nchi hiyo inayotawaliwa kwa mfumo wa kifalme.
Wananchi wa Bahrain wanaoshikiliwa katika magereza na korokoro za nchi hiyo wametangaza mara chungu nzima kwamba, wanakabiliwa na mateso makali na kwamba, wamekuwa wakiteswa ili wakiri makosa ambayo kimsingi hawajayafanya. Hatua hizo zinathibitisha kwamba, mahakama za Bahrain hazina hata vigezo vidogo kabisa vya kimataifa za utoaji hukumu kwa uadilifu. Vitendo vya dhulma na ukandamizaji nchini Bahrain vimekithiri kiasi kwamba, Shirika la Kutetea Haki za Binadamu la Human Rights Watch  limeutaja mfumo wa kimahakama nchini humo kwamba, ni " Mfumo Kwa Ajili ya Dhulma" na kusisitiza kwamba, mahakama za nchi hiyo ya Kiarabu zimekuwa na nafasi muhimu katika kuusauidia utawala wa nchi hiyo katika kutekeleza siasa zake za ukandamizaji.
Hamad bin Isa Al Khalifa, mfalme wa Bahrain
Kwa hakika matukio ya Bahrain yanabainisha uhakika huu kwamba, kuna ukandamizaji mkubwa kabisa unaofanywa na utawala wa Aal Khalifa dhidi ya wananchi wa nchi hiyo. Kamatakamata na utiaji mbaroni ni vitendo ambavyo vimekuwa vikichukua mkondo mpana zaidi na wa kutia wasiwasi. Hukumu za kidhalimu dhidi ya wanaharakati wa kisiasa zinaendelea kutolewa nchini Bahrain katika hali ambayo, ripoti kutoka nchini humo zinaonyesha kuwa, kwa sasa kuna zaidi ya wanaharakti elfu kumi katika magereza ya Bahrain huku 150 kati yao wakiwa wamehukumiwa kifungo cha maisha jela.
Ukiukaji wa haki za binadamu wa utawala wa Aalha Khalifa umeigeuza nchi hiyo na kuifanya kuwa gereza kubwa. Kama ilivyokuwa huku nyumba, utawala wa Baharin umeendelea kupata himaya na msaada wa Saudia katika hatua zake za ukandamizaji dhidi ya raia. 
Tangu Februari mwaka 2011, Bahrain imekuwa ikishuhudia maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga utawala wa Aal Khalifa. Matakwa makuu ya Wabahrain ni kuwepo utawala wa kisheria, kukomeshwa ubaguzi wa kimadhehebu, kufanyika mageuzi ya kisiasa na kuheshimiwa haki za binadamu. Matakwa na madai hayo ya kiraia ya wananchi wa Bahrain yanamaanisha kupoteza uhalali wa kutawala utawala wa kifamilia wa Aal Khalifa. Hata hivyo matukio ya Bahrain yanaonyesha kuwa, hatua ya utawala wa Manama ya kusimama kidete mkabala na matakwa halali ya wananchi ni kufuata njia ya madikteta wa zamani kama Kanali Muammar Gaddafi wa Libya, Hosni Mubarak wa  Misri, na Zeinul Abidiin wa Tunisia; njia ambayo haina natija nyingine ghairi ya kukumbwa na ghadhabu za wananchi na mwisho wa usiku ni kudhalilika.

No comments:

Post a Comment