ARUBAINI, MJUMBE WA UMOJA WA KIISLAMU DUNIANI (4)

Arubaini, Mjumbe wa Umoja wa Kiislamu Duniani
Assalaamu Alaykum wasikilizaji wapenzi. Karibuni katika makala hii maalumu tuliyokuandalieni kwa mnasaba wa kumbukumbu ya Arubaini ya Imam Husain AS. Ni mfululizo wa makala maalumu ambazo zinakujieni katika kipindi cha siku hizi kadhaa za kuelekea kwenye kilele cha kumbukumbu hizo zinazofanyika Karbala nchini Iraq ambapo kwa mwaka huu itakuwa ni Jumatatu ya tarehe 21 Novemba kulingana na mwandamo wa mwezi nchini Iraq. Karibuni.
Wanavyuoni wengi wa dini tukufu ya Kiislamu, wanamuhesabu Imam Husain AS kuwa ni moja ya njia kuu za kuleta umoja na mshikamano kati ya umma wa Kiislamu. Mapenzi makubwa ya Waislamu kwa Imam Husain AS hayawahusu Waislamu wa Kishia tu, bali huyo ni kipenzi cha Waislamu wote.
Kuna hadithi nyingi za Mtume Muhammad SAW zinazoonesha utukufu wa kipenzi chake huyo na kusisitiza kuwa Imam Husain AS ni wa Waislamu wote. Miongoni mwa hadithi maarufu ni zile zinazosema, Hassan na Hussein ni mabwana wa vijana wa peponi, Husain anatokana na mimi na mimi ninatokana na Husain, Mwenyezi Mungu mpende anayempenda Husain na  Husain ni merikebu ya wokovu na taa ya uongofu na hadhithi nyinginezo nyingi. Sisitizo lote hilo la Bwana Mtume Muhammad SAW linaonesha kuwa Imam Husain ni wa Waislamu wote, si wa Waislamu wa Kishia pekee na kumpenda Husain ni wajibu uliohimizwa mno na Bwana Mtume. Maana ya kumpenda mtu nako kama tunavyojua, ni kufurahishwa na linalomfurahisha mtu huyo na kuhuzunishwa na linalomuhuzunisha. Arubaini ya Imam Husain AS ni kumbukumbu ya siku ya arubaini tangu tarehe 10 Muharram, aliyouawa shahidi mtukufu huyo katika jangwa la Karbala mwaka 61 Hijria. Hiyo ni siku ambayo wapenzi wa Husain na Bwana Mtume Muhammad SAW wanakusanyika kwa mamilioni huko Karbala Iraq kuomboleza kuuliwa kikatili mjukumuu huyo wa Mtume mwaka 61 Hijria. Naam, Arubaini ya Husain ni mjumbe wa umoja na mshikamano baina ya Waislamu wote.
Husain AS ni merikebu ya wokovu na taa ya uongofu

Kama tulivyotangulia kusema, wanavyuoni wengi wa dini tukufu ya Kiislamu, wanamuhesabu Imam Husain AS kuwa ni moja ya njia kuu za kuleta umoja na mshikamano kati ya umma wa Kiislamu. Mapenzi makubwa ya Waislamu kwa Imam Husain AS hayawahusu Waislamu wa Kishia tu, bali huyo ni kipenzi cha Waislamu wote. Hivi sasa njia na mabarabara ya kuelekea Karbala nchini Iraq yamejaa Waislamu wa madhehebu mbalimbali bali hata wasio Waislamu, kuelekea kwa mahbubu wao kwa kiu na shauku kubwa. Machofu ya safari hayana nafasi kwa maashiki hao. Naam, Waislamu wote wanampenda Imam Husain AS kwa kuwa ni mjukuu wa Mtume Muhammad SAW bali ni sehemu ya mwili wa mtukufu huyo na wanawahesabu wauaji wa Imam Husain kuwa ni watu waovu kabisa. Yazid mwana wa Muawiya alikuwa maarufu kwa maadili maovu na kutoshikamana na dini, na si kwamba alidhulumu haki ya Ahlul Bayt wa Bwana Mtume pekee bali alifanya dhulma nyingine nyingi na kuua kikatili mno Waislamu na maswahaba wa Bwana Mtume Muhammad huko Madina na kuwavunjia heshima wanawake wa Kiislamu. Mauaji hayo maarufu yanayojulikana kwa jina la mauaji ya Harrah yalifanywa na jeshi la Yazid dhidi ya Waislamu wa Madina na masahaba wa Bwana Mtume Muhammad SAW muda mchache baada ya kufanya mauaji ya kutisha dhidi ya mjukuu wa Bwana Mtume yaani Imam Husain AS. Tab'an kipindi hiki si kwa ajili ya kuzungumzia jinai zilizofanywa na Yazid, hivyo hatutosema mengi kuhusiana na suala hilo. Tulichokusudia kusema tu ni kuwa Imam Husain AS alisimama kupambana na mtu ambaye kivuli kiovu cha dhulma na ufisadi wake kiliwatesa Waislamu wote bila ya kubagua, na utawala wake wa kiimla ulilenga moja kwa moja kuaangamiza Uislamu na sunna za Bwana Mtume Muhammad SAW. Hivyo mtazamao wa maulamaa wakubwa wa dini ya Kiislamu kutoka madhehebu mbalimbali ni wajibu wa kumpenda Imam Husain AS na mapenzi hayo ni nukta inayoyaunganisha madhehebu yote ya Waislamu.

Kama tutazingatia kidogo tu aya za Quráni Tukufu na hadith za Bwana Mtume SAW tutaona kuwa, dini tukufu ya Kiislamu imehimiza mno suala la umoja na mshikamano baina ya Waislamu, kiasi kwamba Quráni Tukufu inawataka Waislamu kujiepusha kuingia katika mizozo na malumbano, hata na wasiokuwa Waislamu ili isiwe sababu watu hao kumtukana Mwenyezi Mungu kiuadui na kuwa sababu ya kujenga uhasama baina yao na Waislamu. Waislamu wamehimizwa mno kujiepusha na vita hata na watu ambao si Waislamu lakini si maadui. Mwanachuoni maarufu Kashiful Ghitaa ambaye ni mmoja wa maulamaa wakubwa sana na marajii wa karne ya 13 Hijria katika ulimwengu wa Kishia ameandika hivi: Uislamu umeundwa juu ya maneno mawili makuu:  کلمه التوحید و توحید الکلمه Yaani Neno la Tawhidi na Kuunganisha Umma au kwa maneno mengine ni kuwa Uislamu umeundwa kwa maneno mawili, tawhidi na mshikamano. Tawhidi ikiwa na maana ya kumwabudu Mwenyezi Mungu Peke Yake bila ya kumshirikisha na chochote katika hali yoyote ile, na mshikamano una maana ya kuleta umoja katika jamii ya Kiislamu. Amma katika aya ya 105 ya Surat Aal Imran, Mwenyezi Mungu anawakataza Waislamu wasifarikiane kwa kuwambia: Wala msiwe kama wale waliofarikiana na kukhitalifiana baada ya kuwafikia hoja zilizo wazi. Na hao ndio watakaokuwa na adhabu kubwa. Naye Bwana Mtume Muhammad SAW amenukuliwa akisema, Hakuna umma wowote uliozozana baada ya Mtume wao ila kundi la batili liliwafunika wenye haki.
Moja ya baraka za umoja kati ya Waislamu bali hata kati ya watu wowote wale ni kuweza watu hao kuishi kwa salama na utulivu mkubwa na kupitia utulivu huo huweza kuchanua vipaji vya watu wa jamii hiyo na kuwafanya watende mambo yao kimantiki. Mshikamano huo unapokuwa ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, waja wema huweza kuongoza mambo ya jamii hiyo na kuwa sababu ya mafanikio ya duniani na Akhera. Lakini mizozo na mifarakano ni sawa na moto unaowasha na kuteketeza mavuno yote ya mwanadamu na hatimaye kuishia kwenye moto wa adhabu ya Mwenyezi Mungu kwani mizozo huipokonya jamii fursa ya kufikia kwenye ukamilifu wake wa kibinadamu na hivyo kuwa sababu ya kumwasi Mola wao Muumba.

Tunapotupia jicho kidogo tu matunda mazuri yasiyo na kifani ya umoja na mshikamano baina ya Waislamu bilioni moja na nusu duniani tutapata kiurahisi sana majibu ya kwa mini maadui wa Uislamu wana woga na kiwewe kikubwa cha kufikiria tu mshikamano wa Waislamu. Na hiyo ndiyo sababu inayowafanya wafanye kila wanaloweza kuhakikisha kuwa mizozo na ugomvi haumaliziki katika safu za Waislamu. Hivi sasa pia waistikbari na maadui wa Uislamu wameongeza njama zao kuliko wakati mwingine wowote kwa ajili ya kuwagombanisha Waislamu na kujenga uadui mkubwa baina ya madhehebu mbalimbali ya Waislamu. Leo hii umma mkubwa wa Waislamu unahitajia mno umoja kwa ajili ya kujiokoa kutoka katika mateso ya kila namna wanayofanyiwa katika kila kona ya dunia. Mateso ya Waislamu leo hii yanashuhudiwa kila mahali, kuanzia Myanmar hadi katika nchi za Iraq, Syria, Yemen, Bahrain, Nigeria na sehemu nyingine nyingi ulimwenguni. Katika mazingira kama haya, njia iliyooneshwa na Imam Husain AS ambaye alijitolea kila kitu chake kwa ajili ya kupigania haki na kuulinda Uislamu, inarejesha matumaini kwa Waislamu ya kuweza kushinda dhulma zote hizi zilizoukumba umma wa Kiislamu leo hii. Njia hiyo ya Imam Husain AS ambayo ndiyo njia ya babu yake; Bwana Mtume Muhammad SAW ya kusimama imara kupigania haki, ni nukta muhimu mno ya kuwaunganisha Waislamu wa madhehebu yote ambao kama tulivyotangulia kusema, wote wanakubaliana juu ya wajibu wa kumpenda mjukuu huyo wa Bwana Mtume. Njia iliyooneshwa na Imam Husain AS inaleta nuru kila pale ambapo giza linaonekana kukaribia kufunika haki. Arubaini ya Imam Husain AS ni fursa nyingine kwa wanadamu ya kuweza kurudi kwenye dhati yao, naam, kila dhati ya mwanadamu imeumbwa kupenda haki na kuchukia dhulma.
Arubaini, Mjumbe wa Umoja wa Kiislamu Duniani 

Hivi sasa katika nchi ya Waislamu ya Iraq, kwa miaka mingi wakazi wake wanaishi katika mazingira ya ukosefu mkubwa wa amani na vitendo vya kigaidi. Hivi sasa wimbi kubwa la mamilioni ya watu linaendelea kukusanyika nchini humo likijiandaa kwa ajili ya kumbukumbu ya Arubaini ya Imam Husain AS. Huo ni mkusanyiko mkubwa zaidi wa watu duniani kila mwaka. Waislamu wa madhehebu mbalimbali, bali hata wasio Waislamu hushiriki katika safari ndefu ya kutoka Najaf kwa miguu hadi Karbala, tajiriba ambayo mtu yeyote hawezi kuilezea kwa maneno ila yule aliyeshiriki kwenye maandamano hayo ya mamilioni ya watu. Maandamano hayo yanakusanya watu wa rika zote, watu wa daraja za kila aina katika jamii bali ukitoa Waislamu wa Kishia, Waislamu wengi wa Kisunni, na pia Wakristo na wafuasi wa dini nyinginezo hujumuika pamoja kwenye maandamano hayo. Hata hivyo maadui wanaeneza uongo mwingi kuhusiana na maandamano hayo. Bali pia wanatenga fedha nyingi kuyasaidia magenge ya kigaidi kama vile Daesh kueneza chuki baina ya Waislamu. Wanapandikiza fikra ya kwamba hakuna uwezekano wowote wa Waislamu kuwa kitu kimoja na wanakabiliana na juhudi yoyote ile ya kuleta mshikamano baina ya Waislamu. Maadui wanafanya njama za kila namna kuwazuia Waislamu wasishiriki katika kumbukumbu za Arubaini ya Husain AS na kumbukumbu nyingine za Karbala kwani kadiri kumbukumbu hizo zinavyopata nguvu, ndivyo umma wa Kiislamu unavyozidi kuwa imara kwa kumfanya kipenzi huyo wa Bwana Mtume ruwaza njema ya kupambana na dhulma kwa hali yoyote ile. Hata hivyo pamoja na kuweko njama zote hizo za maadui, mvuto wa kipekee wa Imam Husain AS unazivutia nyoyo za wapenda haki na kuzifanya ziweke pembeni tofauti zao zote ndogo ndogo na kuungana katika mapenzi ya maashuki na mahbubu wao huyo.
Waislamu wa Kisunni wakishiriki katika maandamano ya Arubaini ya Husain AS

Barabara za kuelekea Karbala hivi sasa zimejaa vituo ambavyo watu wa kila namna wa kujitolea, wametenga muda wao wote kuwahudumia maashiki wa Husain AS. Wahudumu wakuu wa wafanya ziara hao ni wanavijiji wa Iraq ambao wanajitolea kila kitu chao kuwahudumia wageni hao wa Imam Husain AS. Fukuto la mapenzi kwa Imam Husain AS limewafanya wanavijiji hao kwa nyoyo safi kujitolea kila walicho nacho kupiga kambi katika barabara za kuelekea Karbala ili kupata baraka za kuwahudumia maashiki wenzao wa Imam Husain AS. Cha kuvutia zaidi ni kuwa Waislamu hao si wa madhehebu ya Kishia tu, bali Waislamu wa madhehebu ya Kisuni nao hawako nyuma katika jambo hilo tukufu. Naam, Husain AS ni wa Waislamu wote, bali ni wa kila mpigania haki duniani. Hata Wakristo nao utawaona wanapiga kambi katika barabara za kuelekea Karbala na kuvipa jina la Masih Isa AS vituo vyao vya kuwahudumia wageni wa Imam Husain AS. Wakristo hao wanasema kuwa, Imam Husain AS anatuhusu sote. Misafara ya Waislamu wa Kishia kutoka Pakistan, India na Afghanistan huwa inalazimika kupitia nchini Iran kwa ajili ya kujiunga na wimbi kubwa la maashiki wa Husain wanaoelekea Karbala. Wakati wanapoanza safari yao ya kuingia Iran, huwa wanapitia maeneo ya Waislamu wa Kisuni, na wakati wanapoingia katika ardhi ya Iran huwa wanapokewa kwa mapenzi makubwa na Waislamu wenzao wa Iran wa madhehebu ya Kisuni na huu ni katika muujiza wa mvuto wa mjukuu huyo wa Bwana Mtume SAW ambaye mapambano yake yameziteka nyoyo za wanadamu na kuwa nguzo ya mshikamano baina yao. 

Kwa kweli ni vigumu mno kuitolea maelezo mandhari ya kipekee ya watu wa makabila, mataifa, rika, madhehebu na dini tofauti wanaojumuika pamoja na kukubali mashaka na tabu nyingi za safari na hatari za kiusalama za kushambuliwa na magaidi kwa ajili ya kwenda kumzuru mjukuu wa Bwana Mtume Muhammad SAW Imam Husain AS huko Karbala Iraq. Bila ya shaka ni kwa sababu hii ndio maana Ahlul Bayt wa Mtume Muhammad SAW wamewahimiza sana wafuasi wao kulipa umuhimu mkubwa suala la kumzuru Imam Husain AS. Kwani mtu anapokuwa na welewa sahihi kidogo tu kuhusiana na mtukufu huyo, welewa huo huujaza moyo wake mapenzi makubwa sana kwa Husain AS na ndio maana leo hii, kadiri siku zinavyopita, kumbukumbu za Imam Husain AS hususan Arubaini zinavutia nyoyo za watu wengi zaidi tena kwa mamilioni kutoka kona zote za dunia na haijalishi ni watu wa madhehebu na dini gani, muhimu ni kuwa wawe wapenda haki na ni maadui wa batili, na huo ni uthibitisho tosha kwamba Arubaini ya Imam Husain AS ni mjumbe wa umoja wa Kiislamu, ulimwenguni.  Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

0 comments: