UNICEF: ASILIMIA 60 YA WAKIMBIZI WA ROHINGYA NI WATOTO WADOGO

UNICEF: Asilimia 60 ya wakimbizi wa Rohingya ni watoto wadogo
Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (UNICEF) umetangaza kuwa, karibu asilimia 60 ya wakimbizi Waislamu wa jamii ya Rohingya waliokimbilia Bangladesh kutokana na mauaji na ukatili unaofanywa na Mabudha na jeshi la Myanmar, ni watoto wadogo.
UNICEF imetangaza kuwa, hadi sasa watoto 1400 wa Waislamu wa Rohingya wamesajiliwa baada ya kuvuka mpaka na kuingia Bangladesh wakiwa peke yao bila ya wazazi au wasimamizi wao. 
Taarifa ya UNICEF imesema kuwa, watoto hao wakimbizi wameshuhudia kwa macho mauaji ya wazazi na watu wa familia zao au kuchomwa moto makazi na nyumba zao. 
Taarifa hiyo imeongeza kuwa, kambi za wakimbizi za Waislamu wa Rohingya nchini Bangladesh zina hali mbaya sana na kwamba makumi ya maelfu ya wakimbizi hao wanaoshi katika maeneo yasiyo na usalama na yasiyofaa kwa ajili ya watoto.
Wakimbizi wa Rohingya, Myanmar
Maelfu ya Waislamu wa jamii ya Rohingya wameuawa katika mashambulizi yanayoendelea kufanywa na Jeshi la Myanmar na Mabudha wenye misimamo ya kuchupa mipaka hususan katika jimbo la Rakhine.   
Wimbi jipya la mauaji ya Waislamu wa Rohingya katika jimbo hilo lililoko magharibi mwa Myanmar lilianza tarehe 25 Agosti mwaka huu. Takribani Waislamu laki nne kutoka Myanmar wamekimbilia nchi jirani ya Bangladesh na hali katika kambi za wakimbizi ni mbaya kutokana na kukosekana misaada ya kutosha. 

0 comments: