ONGEZEKO LA UTUMIAJI WA WANAWAKE WA KIAFGHANI KATIKA MAGENDO YA DAWA ZA KULEVYA

Ongezeko la utumiaji wa wanawake wa Kiafghani katika magendo ya dawa za kulevya
Msemaji wa Idara ya Kupambana na Magendo ya Dawa za Kulevya nchini Afghanistan amesema kuwa kumekuwepo ongezeko la utumiaji wa wanawake wa Kiafghani katika magendo ya dawa za kulevya.
Khaled Muvahhed ametaja umaskini, ujinga, matatizo ya kiuchumi na kulazimishwa na watu wa familia kuwa ni miongoni mwa sababu za wanawake wengi wa Afghanistan kujielekeza katika biashara haramu na magendo ya dawa za kulevya. Ameongeza kuwa, katika miezi 11 iliyopita askari usalama wa Afghanistan wamewatia nguvuni makumi ya wanawake kwa tuhuma za kujihusisha na magendo ya dawa za kulevya.
Mbali na sababu zilizotajwa kuwa zinawasukuma wanawake wa Afghanistan katika magendo ya dawa za kulevya, lakini pia inatupasa kusema kuwa, suala hilo ni kielelezo cha kuongezeka sana uzalishaji wa dawa hizo nchini Afghanistan na jitihada za magenge ya mafia ya utoroshaji wa dawa hizo kwa ajili ya kupata njia mpya za biashara hiyo.  
Wanawake wa Afghanistan wametumbukizwa zaidi katika uraibu wa mihadarati
Mafanikio ya kiwango fulani ya serikali ya Afghanistan katika kufunga baadhi ya njia za kusafirisha dawa za kulevya yameyalazimisha magenge ya mafia ya mihadarati kutafuta njia mpya za magendo ya dawa hizo na kulenga zaidi tabaka la wanawake. Suala hili, badala ya kuhusishwa na serikali ya Afghanistan, linafungamana zaidi na sera za madola ya kikoloni kama Marekani na Uingereza huko Afghanistan. Nchi hizo zimetengeneza mazingira ya kustawisha zaidi uzalishaji wa dawa za kulevya na magendo ya dawa hizo huko Afghanistan na kutatiza sana uchumi wa nchi hiyo. Nchi hizo pia katika upande wa pili zinafanya njama za kuangamiza jamii ya Afghanistan hususan kizazi cha vijana wa nchi hiyo kupitia njia ya kuwatumbukiza katika uraibu wa mihadarati na ukweli huo unathibitishwa na takwimu zinazosema kuwa, katika kipindi cha chini ya miongo miwili ya udhibiti wa Marekani huko Afghanistan, zaidi ya raia milioni tatu wa nchi hiyo wamekuwa wateja na waraibu wa dawa za kulevya.
Vijana wa Afghanistan wameathiriwa sana na dawa za kulevya
Mtaalamu wa masuala ya siasa wa Afghanistan, Sayyid Wahiid Dhuhuri Hussaini anasema: Marekani na muungano wa kijeshi wa NATO unatumia jiografia ya Afghanistan kwa ajili ya kukidhi mahitaji yao na kuhakikisha kwamba, dawa za kulevya zinazalishwa nchini humo bila ya kizuizi chochote. Nchi hizo zinasafirisha baadhi ya dawa za kulevya zinazozalishwa Afghanistan na kuzipeleka katika nchi nyingi kwa ajili ya kudhamini mahitaji ya madawa ya nchi za Marekani na Ulaya na jamii ya Afghanistan ndiyo inayodhurika na kupata hasara kubwa zaidi kutokana na dawa hizo za kulevya."
Askari wa Marekani wakilinda mashamba ya zao la mihadarati, Afghanistan
Marekani na Uingereza ambazo ndizo zinazodhibiti hali ya mambo nchini Afghanistan zimeyawezesha makundi ya waasi na ya kigaidi kudumisha harakati zao nchini humo kwa kuyapa uhuru wa kuzalisha fedha kupitia magendo ya dawa za kulevya. Makundi hayo ya kigaidi ambayo daima yanahudumia malengo ya siasa za kikoloni za Marekani na washirika wake, hivi karibuni yaliingia vitani na katika mapigano ya wenyewe kwa wenyewe ya kudhibiti maeneo yenye hali bora zaidi kwa ajili ya kuzalisha dawa za kulevya na mihadarati. Mtaalamu wa siasa wa Russia, Anatoly Maradasov anasema: "Sababu ya hitilafu na mapigano ya kundi la Taliban na Daesh huko Afghanistan ni kutaka kudhibiti mikoa inayozalisha kwa wingi dawa za kulevya na kunyang'anyana tonge hilo nono."
Alaa kulli hal, kutumbukizwa wanawake katika magendo na usafirishaji wa dawa za kulevya nchini Afghanistan ni matokeo ya karibu miongo miwili ya kuwepo kwa majeshi ya Marekani na Uingereza nchini humo. Nchi hizo mbili na washirika wao wanavunja nguzo za usalama na amani ya Afghanistan na nchi jirani kupitia njia ya kusaidia ustawishaji wa dawa za kulevya nchini humo.

0 comments: