KUWASILI kwa watalii 65 kwa treni inayoshikilia nafasi ya pili kwa ufahari duniani Rovos Rail, kumeendelea kuiweka Tanzania katika ramani nzuri kama sehemu salama kwa utalii na mapumziko.

Akizungumza wakati wa mapokezi hayo katika kituo cha TAZARA jijini hapa, Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Devota Mdachi amesema fursa kama hizi zinapojitokeza ni wakati wa kuonyesha ukarimu watanzania.

“Sisi ndio wenyeji wao lazima tuonyeshe hawakukosea kuchagua kuja Tanzania, hivyo nawaasa wananchi kuwapa mapokezi mazuri na kuwakirimu wageni hawa ambao wengine watakwenda Zanzibar na wengine watabaki hapa kwa siku kadhaa kabla ya kuondoka,” alisema Bi. Mdachi na kusisitiza:

“Tanzania ina vivutio vingi, kama nilivyowahi kueleza siku za nyuma treni hii ambayo imeanza safari yake katika mji wa Pretoria Afrika wiki kadhaa zilizopita na kukanyaga reli ya TAZARA katika kituo cha Kapiri Mposhi nchini Zambia Julai 11, kisha ikakanyaga ardhi ya Tanzania Julai 12 imepitia vituo kadhaa vya kiutalii ikiwemo Mbuga ya Selous.”

TTB ipo katika mazungumzo na uongozi wa TAZARA ili kutumia nafasi ya wageni wanaotoka mataifa mbalimbali kujifunza utamaduni wa Tanzania pamoja na kutembelea vivutio vya kiutalii ili wanaporejea katika mataifa yao kuelezea uzuri wa nchi hii.

Akielezea namna alivyofurahishwa na vivutio vya Tanzania, mmoja wa abiria wa treni hiyo ambaye pia ni daktari wa abiria, Dkt. Hester Wannenburg alisema: “Hii ni mara yangu ya kwanza kuja Tanzania njiani nimeona mambo mengi mazuri ya kuelezea. Wanyama na maporomoko ya maji ni vitu ninavyovipenda. Nimefurahi kuwepo Tanzania na naamini nitarejea tena.”

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Bwana Martin Loibooki amesema watalii hao wanakuja zaidi ya mara mbili kwa mwaka na wameonyesha kuvutiwa na mbuga ya Selous, hivyo wanatafuta namna ya kuwafanya wakae zaidi katika mbuga hiyo.

“Tupo katika mazungumzo na uongozi wa TAZARA ili treni hii ya kitalii na nyinginezo zikae kwa muda walau siku moja katika pori la Selous, ndicho kitambulisho chetu katika ukanda huu kwa sababu ni mbuga yenye wanyama wengi na vivitio vingi zaidi,” alisema Bw. Loibooki.

Treni hiyo ya kifahari hufanya safari zake kati ya Pretoria Afrika Kusini na Dar es Salaam mara nne kwa mwaka ambapo asilimia kubwa ya abiria wanaopanda ni wastaafu kutoka mataifa mbalimbali ulimwenguni. Hupanda kuanzia Pretoria na kupitia Botswana, Zimbabwe, Zambia na hatimaye Tanzania.

Bodi ya Utalii nchini ni miongoni mwa taasisi zinazopambana kuhakikisha Tanzania inatambulika kimataifa kupitia vivutio vyake na utamaduni, kwa kipindi kirefu sasa bodi hiyo imekuwa ikifanya kazi na sekta mbalimbali ikiwemo za usafari na michezo.

0 comments: