MWILI WA MZEE FRANCIS MAIGE KANYASU ‘NGOSHA’ WASAFIRISHWA LEO

Mwili wa marehemu Mzee Francis Maige Kanyasu  umeagwa leo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)  na kusafirishwa na serikali kwenda kijijini kwao Igokero wilayani Misungwi.


Shughuli ya kuuaga mwili huo imeongozwa na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya , Maendeleo ya Jamaii , Jinsia , Wazee na Watoto, Marcel  Katemba ambaye amemwakilisha Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk. Mpoki Ulusubisya.

Akizungumza katika shughuli hiyo Bwana Katemba ameipongeza Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa jitihada kubwa walizofanya za kumpatia tiba na kumuhudumia kwa kipindi alichokuwa amelazwa  hospitalini hapo.

“Nawapongeza Muhimbili kwa juhudi zenu ni kweli mlitaka kuokoa maisha ya mzee wetu, lakini kazi ya Mungu haina makosa , pia sina budi kuwashukuru majirani zake na uongozi wa Serikali ya Mtaa wa Malapa kwa kujitoa naomba mfanye hivyo hata kwa wazee wengine’’ amesema Katemba.

Naye Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Dharura na Ajali, Dk. Juma Mfinanga amesema walimpokea Mzee Kanyasu Mei 25, 2017 akitokea Hospitali ya Amana alikokua akipatiwa matibabu na walipomfanyia vipimo vya awali waligundua kwamba ana maradhI ya Kifua Kikuu ambayo alikuwa nayo kwa muda mrefu kutokana na mazingira aliyokua akiishi.

Hivyo Dk. Juma ametoa rai kwa wananchi kujenga tabia ya kwenda hospitalini mapema pindi mtu anapoona hali yake ya kiafya si nzuri kwani ukiwahi hospitali ni rahisi kupata  tiba na kupona kuliko kusubiri hadi ugonjwa uwe sugu.

Mzee Francis Maige Kanyasu alizaliwa 1931 na kufariki dunia Mei 29 , 2017 saa mbili na nusu usiku katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Baadhi ya wawakilishi kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wakiaga mwili wa marehemu Francis Maige Kanyasu (86) katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) leo. Marehemu alikuwa amelazwa katika hospitali hiyo na wakati akiendelea na matibabu mauti yakamkuta.
Mwili wa marehemu ukiwa umebebwa tayari kwa safari ya kuelekea Misungwi mkoani Mwanza ambako mazishi yatafanyika. 0003: Baadhi ya wafanyakazi wa Muhimbili wakisubiri kuuaga mwili huo leo. Kulia ni Zuhura Mawona ambaye amemwakilisha Mkurugenzi wa Uuguzi, Agness Mtawa na Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji, Dk Julieth Magandi.
Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Marcel Katemba ambaye amemwakilisha Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk Mpoki Ulusubisya akizungumza kabla ya shughuli za kuaga mwili huo leo.

Baadhi ya watu waliofika kuaga mwili huo leo.
Mkurugenzi wa Huduma na Upasuaji wa Muhimbili, Dk Julieth Magandi akiwashukuru watu mbalimbali walofika kuuaga mwili huo leo.
Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Dharura na Ajali wa Muhimbili, Dk Juma Mfinanga akieleza jinsi Hospitali ya Muhimbili ilivyokuwa ikimpatia matibabu mzee Francis Maige Kanyasu.

0 comments: