MAMBO YA KUJICHUNGA KATIKA MWEZI MTUKUFU WA RAMADHANI

Assalamu alaykum warahmatullahi wabarakatuh. Karibuni wasomaji wapenzi katika wakati huu maalumu nilichokuandalieni kwa mnasaba wa mwezi mtukufu wa Ramadhani ambacho  kitaanza kwa kugusia falsafa na hekima ya funga.
Kuhusu falsafa na hekima ya funga au saumu yamezungumzwa mengi ndani ya Qur’ani tukufu, Hadithi pamoja na kauli za maulamaa wa dini. Katika kubainisha hukumu ya kufaradhishwa na kuwajibishwa kufunga, Qur’ani tukufu imeitaja taqwa na ucha Mungu kuwa moja ya hekima za kufaradhishwa amali hiyo tukufu. Aya ya 183 ya Suratul Baqarah inasema:

Enyi mlio amini! Mmeandikiwa Saumu, kama walivyo andikiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kuchamungu.

Funga ni moja ya amali bora kabisa za kumwezesha muumini kudhibiti ghariza za kihayawani na kuhuisha moyo wa uchaji Mungu ndani ya nafsi yake. Kama ilivyoelezwa katika Hadithi ni kwamba:

 “Funga ni ngao (ya Moto wa Jahannamu)”. Yaani mtu atanusurika na kuokoka na Moto wa Jahannamu kutokana na kufunga. Na sababu ni kuwa, kutokana na t’aa, ibada anazofanya mtu na kuzidhibiti na kuzidhoofisha hawaa na matamanio ya nafsi hatimaye huweza kumdhibiti na kumshinda shetani wa ndani na nje ya nafsi yake.

 Na ni kutokana na hayo ndipo Bwana Mtume Muhammad (S.A.W) akasema: “Ndani ya mwezi huu mashetani hufungwa pingu na minyororo, basi mwombeni Mwenyezi Mungu asiwasalitishe juu yenu”.
Wapenzi wasomaji, katika mambo yanayomshawishi na kumsukuma mtu kwenye matendo mabaya na maovu, la kwanza kabisa ni “nafsun ammarah” yaani nafsi inayoamrisha mabaya na hawaa za nafsi. Kwa hakika kama shetani atataka kumhadaa mtu, basi hufanya hivyo kupitia nafsi inayoamuru kufanya mabaya. 

Katika mwezi mtukufu wa Ramadhani, kutokana na kufunga, kuomba dua na kutekeleza ibada nyengine mbalimbali, Waislamu wengi hujitahidi kujiongezea sifa bora za kiakili kwa upande wa imani safi na tabia njema na vilevile kubadilisha mwenendo wao wa kidini katika uga wa masuala ya kijamii.

 Mchanganyiko na muongezeko wa imani na muelekeo wa kidini katika mwezi mtukufu wa Ramadhani huhafifisha na kudhoofisha nafasi ya nafsi inayoamuru kufanya mabaya. Na jambo hilo ndilo linalozuia mno athari za ushawishi wa shetani.

Kwa mujibu wa aya za Qur’ani tukufu, shetani ameapa kuwa atawapotosha na kuwatoa nje ya mkondo wa njia iliyonyooka waja wote wa Mwenyezi Mungu isipokuwa wale ambao ni “mukhlasin”

Kwa hivyo kila mja ambaye anamwomba na kumwabudu Allah kwa ikhlasi, shetani hatokuwa na nguvu juu yake. 
Na sababu ni kuwa, kama ambavyo maji na moto havitangamani, kumdhukuru na kumtaja Allah kunakinzana na wasiwasi wa shetani; na vitu viwili vyenye mgongano haviwezi kujumuika pamoja.

 Kwa hivyo maana ya kufungwa mikono na miguu mashetani kwa minyororo ni kwamba katika mwezi mtukufu wa Ramadhani, dhikri, dua na utajo wa Allah huwa mkubwa na mwingi kiasi ambacho haibakii tena fursa yoyote ile kwa wasiwasi wa shetani aliyebaidishwa na rehma za Allah.

Wapenzi wasomaji, maana ya funga au saumu kilugha ni kujizuia na kila kitu; na katika istilahi za fiqhi maana yake ni kujizuia na mambo manane ikiwemo kula na kunywa kuanzia alfajiri hadi magharibi kwa nia na kusudio la kutekeleza amri ya Mwenyezi Mungu. 

Mtu ambaye amechunga hukumu za dhahiri na za kifiqhi za funga, funga yake huwa imesihi kisheria. Lakini ili funga na saumu yake ikubalike na kupata malipo ya thawabu mbele ya Mwenyezi Mungu kuna masharti yanayomlazimu kutekeleza. 

Funga inayotakabaliwa ni ile inayomjenga na kumkuza mtu kimaanawi. Saumu ya aina hiyo, mbali na kuchunga hukumu za funga, yaani kujizuia na kula na kunywa na mengineyo, huandamana pia na kuviepusha viungo na mambo ya haramu bali pia hata ya makruhu. Ikiwa mfungaji atapata taufiqi ya aina hiyo, funga yake huwa imesihi na amali zake huwa zimetakabaliwa na humuongoza kuelekea kwenye ukamilifu na kumkurubisha na Mwenyezi Mungu.
Bwana Mtume Muhammad SAW amesema: Enyi Waislamu jueni kwamba, si hasha watu wengi wakawa wanasali Sala za usiku lakini hawapati hadhi yoyote kwa kukesha kwao huko isipokuwa mateso ya kukaa macho; na si hasha watu wengi wakawa wanafunga lakini hawapati faida yoyote kutokana na kufunga kwao ghairi ya kukaa na njaa na kiu!”
Maneno haya ya Bwana Mtume yanabainisha kuwa kiwango na wingi wa ufanyaji ibada wa mtu, hauwezi kuwa kipimo cha kuonyesha thamani na utukufu wake na matunda ya juhudi zake; bali ubora na namna ya ufanyaji ibada wa mtu ndio unaoakisi thamani na utukufu wake wa kimaanawi.

Imepokewa Hadithi kwamba wanawake wawili walikuwa wamefunga saumu katika zama za Bwana Mtume Muhammad (S.A.W), lakini ulipokaribia wakati wa kufuturu hali zao zilikuwa taabani kwa kiu na njaa kali. 

Kwa hali hiyo wakamtuma mtu kwa Bwana Mtume S(A.W) akawaombee ruhusa ya kufungua. Bwana Mtume Muhammad (SA.W) aliwapelekea chombo wanawake hao na kumwambia aliyewatuma: “Waambie wavitapike vile walivyovila!” Kilichotokea ni kwamba nusu ya chombo kile ilijaa mapande ya damu na nyama. 

Watu walipatwa na mshangao walipoona hali ile. Bwana Mtume akawaambia: Wanawake hawa walijizuia na yale ambayo yalikuwa halali kwao, na wakabatilisha funga zao kwa yale waliyokuwa wameharamishiwa, kwa namna ambayo walikuwa wakikaa kuwasengenya watu; kwa hivyo hivi vilivyomo ndani ya chombo hiki ndiyo yale waliyokuwa wakiwasema watu!”

Wapenzi wasikilizaji, tujitahidini sana kuzichunga ndimi zetu, macho na masikio yetu na mambo yaliyoharamishwa ili tusije tukawa katika wale ambao hawapati chochote katika funga zao zaidi ya kushinda na njaa na kiu. Wassalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh…/

0 comments: