Viongozi wa Umoja wa Ulaya wanakutana leo Machi 9, 2017
mjini Brussels katika mkutano wa kilele uliogubikwa na ajenda kadhaa
ikiwemo suala la uchaguzi wa Rais wa Baraza la Ulaya.
Mkutano huo wa kilele pia unatarajia kuangazia masuaala mengine ikiwa
ni pamoja na suala linalohusiana na uchumi barani ulaya, hali ya sasa
ya ukanda wa magharibi wa nchi za Balkan pamoja na suala la ulinzi na
ushirikiano wa kijeshi.
Mkutano huo huenda ukawa wa mwisho
viongozi wa Umoja wa Ulaya kukutana kabla ya Waziri Mkuu wa Uingereza
Theresa May kuanzisha rasmi mchakato wa kujitoa kwenye umoja huo kwa
kutumia ibara ya 50 ya mkataba wa Lisbon.
Uingereza inatarajia
kutangaza rasmi kusudio lake la kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya ifikapo
mwishoni mwa mwezi Machi na hivyo kuanza rasmi kipindi cha miaka miwili
cha mchakato wa kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya.
Mkutano huo
unafanyika kukiwa na mvutano kati ya Waziri Mkuu wa Poland,
Beata Szydlo na viongozi wengine wa mataifa yanayounda umoja huo
ambao wanaonekana kuiunga mkono hoja ya Donald Tusk kuendelea tena na
wadhifa huo huku Waziri Mkuu wa Poland akimshutumu Tusk ambaye alitokea
katika chama cha upinzani nchini Poland cha Civic Platform (PO) na
alikuwa afisa wa serikali nchini Poland kwa kujihusisha na siasa za
ndani za Poland.
Hata hivyo kwa upande wake Tusk amesema yuko
tayari na anasubiri uamuzi wa viongozi wa mataifa 28 yanayounda Umoja wa
Ulaya katika kuelekea uchaguzi huo huku pia akikanusha hoja
zilizoibuliwa na waziri mkuu wa Poland, Beata Szydlo kuwa amekiuka
taratibu zake za kazi kwa kuingilia siasa za ndani za Poland.
Tusk
amesisitiza kuwa hausiki hata kidogo na migongano hiyo na kuwa haiegemei
upande wowote na wala hatarajii kufanya hivyo hata katika siku za
usoni.
Serikali ya Poland ambayo haiuangalii kwa jicho jema Umoja
wa Ulaya na ambayo imekuwa ikirumbana na Umoja wa Ulaya juu ya utawala wa
sheria Jumamosi iliyopita ilipendekeza jina la Mbunge wa Ulaya, Jacek
Saryusz- Wolsk kuwania nafasi hiyo badala ya Donald Tusk.
Tusk apewa nafasi kubwa ya kuchaguliwa tena
Rais wa sasa wa baraza la ulaya Donald Tusk
Ujerumani
kwa upande wake imesema kuna dalili njema za kuchaguliwa tena kwa
Tusk ambaye kipindi chake cha sasa cha uongozi kinamalizika mwezi Mei
kuendelea kuwa Rais wa Baraza la Ulaya mnamo wakati wanadiplomasia wa
ulaya wakiishutumu serikali ya Poland kwa kutaka kuhusisha masuala ya
ndani na masuala ya kimataifa.
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema kuchaguliwa kwa Tusk ni ishara ya uthabiti ndani ya Umoja wa Ulaya.
Mvutano
huo kati ya serikali ya Poland na Umoja wa Ulaya unaelekea kuleta
mgawanyiko katika kipindi ambacho viongozi wa umoja huo wametoa mwito wa
kuimarishwa umoja mnamo wakati Uingereza ikijiandaa kuanzisha rasmi
mchakato wa kujiondoa kwenye umoja wa ulaya.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: