SILAHA ZA NYUKLIA ZA UTAWALA WA KIZAYUNI NI TISHIO KWA USALAMA WA DUNIA

Mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) amesema silaha za nyuklia za utawala wa Kizayuni wa Israel ni tishio kwa amani na usalama wa kimataifa na ametaka wakala huo uchunguze na kufuatilia kwa uzito mkubwa mpango wa silaha za nyuklia wa utawala huo.
Reza Najafi ametoa wito huo jana katika siku ya mwisho ya kikao cha msimu cha Bodi ya Magavana wa IAEA, ambapo mbali na kuashiria jinsi nchi wanachama wa Harakati Isiyofungamana na Siasa za Upande Wowote (NAM) zilivyolaani vikali mpango wa silaha za nyuklia wa utawala wa Kizayuni, ametaka suala hilo lizingatiwe kwa makini na kufuatiliwa kwa uzito mkubwa na Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki.
Najafi ameashiria wito uliotolewa mara kadhaa na jamii ya kimataifa kupitia maazimio ya IAEA na mikutano ya kuangalia upya Mkataba wa Kuzuia Uundaji na Uenezaji Silaha za Nyuklia (NPT) wa kuutaka utawala haramu wa Israel ujiunge haraka na mkataba huo na kuweka vinu vyake vya nyuklia chini ya usimamizi na uangalizi kamili wa IAEA na kueleza kuwa, kwa masikitiko, katika miaka yote hii utawala wa Kizayuni, kwa kupuuza wito wa kisheria wa jamii ya kimataifa na kwa uungaji mkono kibubusa wa baadhi ya nchi za Magharibi umeendelea kukiuka waziwazi sheria na kaununi zote za kimataifa na kuendeleza mipango yake ya kijeshi ya nyuklia.
Rais wa Marekani Trump na Waziri Mkuu wa Israel Netanyahu
Mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) amekosoa vikali pia tabia ya kindumakuwili ya baadhi ya nchi za Magharibi kuhusiana na kuzuia ueneaji wa silaha za nyuklia na katika kutekeleza marufuku kamili ya kutoipatia Israel zana na mada za nyuklia, utawala ambao kutokana na historia yake iliyojaa vitendo vya uvamizi, ukaliaji ardhi kwa mabavu na ugaidi wa kiserikali, ni tishio kwa amani na usalama wa dunia.../ 

0 comments: