SHAMBULIO LA KUNDI LA KIGAIDI KWENYE VITUO VYA MAFUTA NCHINI LIBYA
Posted by khamisimussa77@gmail.com at 9:09 PM
Sambamba na kuendelea migogoro ya kisiasa na
kutokuwepo usalama nchini Libya, kwa mara nyingine kundi moja la wabeba
silaha limeweza kudhibiti kituo cha mafuta katika eneo linalojulikana
kwa jina maarufu la 'Hilali ya Mafuta' kaskazini mashariki mwa Libya.
Kundi la wabeba silaha linaloitwa
'Vikosi vya Ulinzi wa Benghazi' limedhibiti kituo hicho muhimu cha
mafuta ingawa hadi sasa bado mapigano yanaendelea. Kundi hilo limesonga
mbele hadi eneo lenye vifaru vya kisasa na rada ya kuzuia mashambulizi
ya anga eneo la uwanja wa ndege wa Ra's Lanuf. Hii ni katika hali
ambayo, miezi michache iliyopita, kwa kuungana makundi ya kijeshi ya
nchi hiyo, yaliweza kuliondoa kundi la kigaidi na ukufurishaji la Daesh,
kutoka maeneo liliyokuwa linayadhibiti. Hata hivyo kuendelea tofauti
baina ya makundi ya kisiasa nchini humo, kumetoa mwanya mpya kwa kundi
la kigaidi la 'Vikosi vya Ulinzi wa Benghazi' kuchukua nafasi ya kundi
la Daesh na kudhibiti kituo hicho cha mafuta.
Wakati huo huo serikali ya umoja wa
kitaifa yenye makao yake mjini Tripol, magharibi mwa Libya, imetangaza
kutohusika na mizozo ya kijeshi katika eneo la Hilali ya Mafuta. Hii ni
katika hali ambayo kikosi cha ulinzi wa vituo vya mafuta nchini Libya
kilicho chini ya kamanda Khalifa Haftar, ambaye ni mkuu wa jeshi la nchi
hiyo na aliye chini ya serikali yenye makao yake mashariki mwa nchi
hiyo, hakiikubali serikali ya umoja wa kitaifa yenye makao yake mjini
Tripoli. Inafaa kukumbusha kuwa, tarehe 12 Septemba mwaka jana, Haftar
aliongoza operesheni kali za kijeshi katika eneo la Hilali ya Mafuta na
kufanikiwa kudhibiti vituo vya mafuta vya Al-Zuwaitina, al-Bariqah, Ra's
Lanuf na al-Sidr. Hivi sasa genge la kigaidi la Vikosi vya Ulinzi wa
Benghazi lenye mafungamano na mtadao wa kigaidi wa al-Qaidah,
linakusudia kuliteka eneo hilo ili lipate fedha za kugharamia operesheni
zake za kigaidi nchini Afghanistan, Misri na hata katika nchi za Ulaya.
Libya ilitumbukia katika mgogoro wa ndani hapo mwaka 2011 baada ya
kuondolewa madarakani serikali ya Kanali Muammar Gaddafi, kufuatia
uingiliaji wa baadhi ya madola ya Kiarabu na Muungano wa Kijeshi wa Nchi
za Magharibi (NATO). Uingiliaji huo ndio uliotoa mwanya wa
kuendelea machafuko ya ndani sambamba na kujipenyeza katika nchi hiyo
yenye utajiri wa mafuta, makundi ya kigaidi likiwemo la Daesh. Libya
inakabiliwa na hatari kubwa hivi sasa hata kwa kuongezeka machafuko ya
muda mrefu sasa, na pia kuweko makundi ya wanamgambo ya kigaidi hususan
katika maeneo yenye migogoro. Isisahaulike kuwa, Libya ni moja ya nchi
muhimu na mzalishaji mkubwa wa mafuta katika soko la dunia. Bajeti yake
inadhaminiwa kupitia nishati hiyo muhimu.
Isisahaulike kuwa, iwapo maeneo hayo ya
yenye utajiri wa mafuta yatatekwa na magenge ya kigaidi, kutazorotesha
mno uchumi dhaifu wa nchi hiyo baada ya jambo hilo kuikatia Libya vyanzo
vyake vya kifedha. Mbali na tishio la makundi ya kigaidi, hivi sasa
Libya inakabiliwa na hatari nyingine ya kugawika vipande vipande. Si
hayo tu, lakini pia mizozo ya kisiasa baina ya makundi tofauti bado
inaendelea. Hadi hivi sasa na licha ya upatanishi wa nchi tofauti za
kieneo wa kuwakutanisha viongozi tofauti wa Libya, lakini bado
hakujafikiwa makubaliano chanya. Ni hivi karibuni tu ambapo bunge na
serikali yenye makao yake huko mashariki mwa Libya, lilikataa pendekezo
la Misri la kutaka kuwa mpatanishi. Vita na mapigano ya ndani ya kuwania
madaraka nchini humo si tu kwamba vimetoa nafasi ya kujistawisha
makundi ya kigaidi, bali pia kumetoa mwanya wa uingiliaji wa masuala ya
ndani kwa nchi za Magharibi na baadhi ya nchi za eneo hilo.
Nchi hizo zinafanya njama sambamba na
kutoa uungaji mkono wa siri kwa makundi ya kigaidi, kuendeleza moto wa
vita na tofauti nchini Libya na hata katika eneo zima la kaskazini mwa
Afrika, ili kwa njia hiyo ziweze kupanua ushawishi wao katika eneo hilo.
Ni kwa ajili hiyo, hujuma iliyoendana na udhibiti wa kituo cha mafuta
cha eneo la Hilal ya Mafuta, kumeyafanya makundi ya kisiasa
kutahadharisha juu ya njama za kuharibu juhudi kwa ajili ya kufikiwa
makubaliano ya usalama na amani nchini humo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: