Na: Lilian Lundo - MAELEZO
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
inatararajia kuanza upasuaji wa kupandikiza Moyo kwa wagonjwa wenye matatizo ya
moyo nchini.
Mkurugenzi wa Upasuaji na Daktari
Bingwa wa Upasuaji wa Moyo na Mishipa ya Damu Dkt. Bashir Nyangasa amesema
hayo leo Jijini, Dar es Salaam alipokuwa akiongea na vyombo vya habari kuhusu
malengo ya Taasisi hiyo.
“Tuko katika maandalizi ya kuandaa mapendekezo kwa ajili ya kupeleka Bungeni ili Bunge
lilidhie na kupitisha sheria itakayoruhusu mtu kuandika wosia wa viungo vyake
kutumika mara baada ya kufariki, ikiwemo moyo, figo na viungo vingine,”
alifafanua Dkt. Nyangasa.
Aliendelea kwa kusema kuwa, umefika
wakati kwa watanzania kujiwekea utaratibu wa kuacha wosia wa kutumika kwa
viungo vyao mara baada ya kufariki kwa ajili ya kuhifadhiwa katika benki za
viungo ili viweze kutumika na watu ambao wanauhitaji.
Aidha Dkt. Nyangasa amesema hospitali
ya Apolo Bangalole ya India na hospitali nyingine za kimataifa za magonjwa ya moyo
kwa sasa zimehamia JKCI kutokana na huduma pamoja na vifaa vinavyopatikana
katika hospitali hizo vinapatikana katika Taasisi hiyo.
Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi
Huduma za Tiba, Daktari Bingwa wa Wagonjwa wa Moyo Dkt. Tulizo Shemu amesema
kwa mwaka 2016 Taasisi imefanya uchunguzi wa tiba kwa wagonjwa 973, kati ya
wagonjwa hao 620 walipatiwa matibabu ya moyo ya bila kufungua kifua kwa kupitia
mishipa ya damu (Catheterization) na wagonjwa 353 walifanyiwa upasuaji wa
kufungua kifua.
Vilevile amesema kuwa kwa mwaka huu
wa 2017 Taasisi hiyo imejipanga kufanya upasuaji wa kupasua kifua kwa wagonjwa
700 na wagonjwa wengine 1000 watafanyiwa
operesheni bila ya kufungua kifua kwa kutumia mtambo wa ‘Catheterization’.
Taasisi hiyo inategemea kuwa na kambi
maalum ya matibabu ya moyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Open Heart
International ya nchini Australia kuanzia Machi 10, 2017 ambapo wagonjwa 25
wakiwemo watoto 15 na watu wazima 10 watafanyiwa upasuaji.
Wananchi wameombwa kujitokeza
kuchangia damu kutokana na uhitaji wa damu nyingi katika upasuaji huo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: