WANAHARAKATI WANAOPINGA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI WAPATA PIGO

Wanaharakati wanaopinga Sheria ya Huduma za Habari iliyopitishwa hivi karibuni wamepata pigo baada ya mmoja wa wakili Bw. Francis Stolla kujitoa katika utetezi.

Akiongea leo Jijini Dar es Salaam Wakili nguli wa Kujitegemea Bw. Stolla alisema kuwa ameamua kujitoa katika kesi hiyo iliyofunguliwa na wanaharakati dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutokana na kukabiliwa na majukumu mengine.

“Wakati Shauri linafunguliwa Arusha sikuwepo kwa sababu ya majukumu mengine, pia lilivyofunguliwa Mwanza sikuwepo hivyo kutokana na hilo nimeamua kuwaachia mawakili wengine waendelee na shauri hilo na mimi niendelee na majukumu mengine” alisisitiza Wakili Stolla.

Alisema kuwa madai makubwa ya mawakili hao ni kwamba Sheria ya Huduma za habari inakiuka mkataba wa Afrika Mashariki, na kusema kuwa kesi iliyofunguliwa Mwanza inaitaka Mahakama itamke kwamba kuna baadhi ya vifungu vilivyotajwa kwenye Sheria ya Huduma  Habari inakiuka Katiba ya nchi.

Akiongea kuhusu dalili za kushindwa kwa kesi hiyo iliyofunguliwa na wanaharakati dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika mahakama ya haki ya Afrika Mashariki na Mahakama kuu Mwanza Bw. Francis Stolla alisema suala hilo anaiachia mahakama kwani ni kinyume kutoa mapendekezo wa kesi kushindwa au kushinda.

“Mara nyingi huwa tunaiachia Mahakama na mashauri hayo yote mawili yapo Mahakamani huwezi sema shauri hili litashinda ama kushindwa kwa sababu mashauri yakiwa mahakamani haturuhusiwi kusema shauri hili litashinda ama kushindwa ili Mahakama ibakie kuwa huru” alisema Wakili Stolla.

Kesi hiyo ilifunguliwa na wanaharakati katika mahakama ya haki ya Afrika Mashariki mkoani Arusha na Mahakama kuu ya Tanzania Mkoani Mwanza.

0 comments: