MAJALIWA ASISITIZA MASHIRIKA YA UMMA KUSHIRIKIANA ILI KULETA MAENDELEO

Image result for majaliwa
Na Daudi Manongi-MAELEZO
Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa amewataka wenyeviti wa Bodi na Wakuu wa Mashirika ya Umma na Mamlaka za udhibiti kuwa wabunifu na kutumia fursa na rasilimali zilizopo nchini ili kuleta maendeleo chanya.
Amebainisha hayo leo Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati akifungua mkutano wa kujadili nafasi ya Mashirika ya Umma katika utekelezaji wa mpango wa pili wa Taifa wa maendeleo wa miaka mitano.
“Rai yangu leo ni kwamba kwenye majadiliano yenu pendekezeni na kufanya mashirika ya umma yawe endelevu,yapanuke zaidi na kuliongezea Taifa mapato na ndio maana nafarijika sana kuona mkutano huu unajumuisha wadau wote muhimu ili pamoja na kuweka mikakati ya namna mashirika ya umma ya Tanzania yanavyoweza kushiriki kwenye utekelezaji wa mpango wa Maendeleo,”Alisema Majaliwa.
Akielezea hali ya mashirika ya umma nchini,Waziri Mkuu amesema kuwa utegemezi wa mashirika unaendelea kupungua na mchango na gawio kutoka kwenye mashirika hayo unaendelea kuongezeka na kuhimiza kuongezeka kwa ubunifu na matumizi mazuri ya rasilimali chache zilizopo na kuongeza kati ya mashirika 65 ya kibiashara,mashirika 8 yanaendeshwa kwa Ruzuku ya Serikali,wakati mashirika 57 hayategemei ruzuku ya Serikali.
Ameagiza kuboreshwa kwa mwongozo wa kupata wajumbe wa Bodi na kuwaagiza kuweka mwongozo rasmi wa namna ya kupata wajumbe hawa kwani ni sehemu inayolalalmikiwa sana na wananchi.
Amesema kuwa wameyashirikisha mashirika ya umma kwenye utekelezaji wa mpango wa maendeleo kwa sababu vipaumbele vya mpango wa pili wa maendeleo wa Taifa wa miaka mitano ambayo ni ujenzi wa viwanda vya kuimarisha kasi ya ukuaji wa uchumi,miradi mikubwa ya kielelezo na miradi wezeshi kwa maendeleo ya viwanda ikiwemo barabara,reli,nishati,bandari maji na mawasiliano.
Aidha ameagiza kuondolewa kwa urasimu katika shughuli za mashirika ya umma kwani unakwamisha uboreshaji na maendeleo ya mashirika ya umma.
Waziri Mkuu pia ametoa rai kwa viongozi wote wa mashirika ya umma kutosaini mikataba isiyo na tija kwa Taifa ambayo inapelekea kupata hasara kubwa na kuhimiza mashirika haya kushirikiana na mashirika ya nje pamoja na sekta binafsi ili kupata nguvu ya pamoja katika kukuza uchumi.
“Ni lazima mashirika ya umma yakafanya kazi kwa pamoja na kwa kushirikiana ikiwemo kubadilishana mbinu na utaalamu ili kulifikisha Taifa hili katika azma yake ya kukuza Uchumi wa viwanda kwa mustakabali wa maendeleo ya nchi yetu”,Alisisitiza Mh.Majaliwa.

0 comments: