WAWILI WAUAWA KWA KUCHOMWA MOTO KWA TUHUMA ZA UJAMBAZI

Watu wawili wanaodhaniwa kuwa majambazi wameuawa kisha kuchomwa moto katika kijiji cha Ifumbo Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya katika jaribio la kufanya uhalifu eneo la machimbo ya dhahabu ya Kasanga Lupa Market. 
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Afisa Mtendaji wa kijiji cha Ifumbo Emily Rajab amesema waliouawa wametambuliwa kwa majina ya Paschaly Paul Simchimba mkazi wa Ileya Lupa Market na Tegemeo Henus mkazi wa Mjele ambapo waliouawa na wananchi waliamua kujichukulia sheria mkononi walipokuwa wakichukuliwa maelezo katika ofisi ya mtendaji. 
Rajabu amesema alitoa taarifa kituo cha Polisi Chunya lakini wakati wakimsubiri kufika wananchi walimtimua Mwenyekiti wa kijiji na yeye kisha kuwafunga kamba majambazi hayo na kuanza kuwapiga kwa silaha mbalimbali kisha kuwachoma kwa kutumia magurudumu ya gari. Polisi walifika walikuta miili imeteketea kabisa. 
Uchunguzi wa awali umeonesha marehemu walikuwa wamehukumiwa kifungo cha miaka thelathini jela mwaka 2014 kwa tuhuma za ujambazi wa kutumia silaha na kusababisha mauaji eneo la Lupa Market ambapo baadaye walitoka.Kwa upande wake mkuu wa Wilaya ya Chunya Rehema Madusa amesikitishwa na tukio hilo ambalo limetokea Ifumbo na kuwataka wananchi kuacha tabia za kujichukulia sheria mkononi kwani wangefikishwa Polisi wangesaidia kubaini mtandao wa ujambazi. 
Baadhi ya ndugu walionekana eneo la tukio wakishuhudia mauaji hayo ambapo Polisi walipofika walichunguza na kuamuru kuzikwa miili hiyo kutokana na kuharibika vibaya .Hakuna mtu yeyote aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo.


MBEYA YETU

0 comments: