PROF. MBARAWA AITAKA NIT KUENDANA NA MAGEUZI SEKTA YA UCHUKUZI
Posted by khamisimussa77@gmail.com at 9:15 AM
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akizungumza na
uongozi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) katika mahafali ya 32
ya Chuo hicho yaliyofanyika jijini Dar es Salaam. Katikati ni Katibu
Mkuu Sekta ya Uchukuzi Dkt. Leonard Chamuriho na pembeni yake ni Mkuu wa
Chuo hicho Prof. Zacharia Mganilwa
Mwenyekiti
wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Prof.
Blasius Nyichomba (kulia), akizungumza na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa katika mahafali ya 32 ya Chuo hicho
yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akihutubia
kongamano la mahafali ya 32 ya Chuo cha Taifa cha Usafirishaji
yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya
wahitimu wa fani za Shahada ya Uzamili, Stashahada ya Uzamili, Shahada
na Diploma katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji wakimsikiliza Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa alipokuwa
akihutubia kongamano la mahafali ya 32 ya Chuo hicho yaliyofanyika
jijini Dar es Salaam.
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akiwatunuku
wahitimu wa fani za Shahada ya Uzamili, Stashahada ya Uzamili, Shahada
na Diploma katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji
Serikali
imekitaka Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), kuboresha mitaala yake
ili kuendana na mageuzi makubwa yanayofanywa katika sekta ya uchukuzi
hapa nchini.
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amesema hayo leo
katika mahafali ya 32 ya Chuo hicho na kusisitiza kuwa Serikali itatoa
nyenzo zote stahiki kwa chuo hicho ili kukiwezesha kutoa wanafunzi
watakaokuwa na soko ndani na nje ya nchi.
“Tumeanza
kufanya mageuzi makubwa katika Sekta ya Uchukuzi ambapo tayari
tumenunua ndege katika mkakati wa kuboresha usafiri wa anga na hivi
karibuni tutaanza ujenzi wa reli ya kisasa (standard gauge),
itakayowezesha treni ya kisasa naya mwendo kasi kutoa huduma kwa kuanzia
Dar es salaam hadi Morogoro”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.
Amesema
reli ya kisasa itakuwa inatumia umeme ili kuwa na mwendo kasi wa
kilomita 160 kwa saa na hivyo kuwezesha usafiri wa Dar es
Salaam-Morogoro kuwa wa chini ya muda wa saa mbili.
Amesisitiza
awamu ya kwanza ya ujenzi wa reli hiyo utaanza hivi karibuni mara baada
ya taratibu za kumpata mzabuni wa ujenzi huo kukamilika.
Amebainisha
kuwa katika mwaka wa fedha ujao, Serikali itatenga fedha kwa ajili ya
kukarabati ujenzi wa miundombinu ya chuo hicho ili kukiwezesha kuwa cha
kisasa na kitakachotoa elimu bora katika ukanda wa Kusini mwa Afrika na
kuhakikisha wahitimu wa fani ya ‘Logistics na Transport
Management’ wanapata bodi ya kitaaluma ili kuratibu fani hiyo .
“Hakikisheni
mnaimarisha utawala bora, utafiti, ushauri wa kitaalamu, machapisho na
huduma yenu iwe ya viwango vya ubora ili kuwezesha wahitimu wenu kupata
soko pindi wanapohitimu”, amesisitiza Prof. Mbarawa.
Prof.
Mbarawa amewataka wahitimu hao kutumia elimu waliyoipata kwa juhudi,
bidii na maarifa ili kuleta manufaa kwao binafsi na Taifa kwa ujumla.
Naye
Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo hicho Prof. Blasius Nyichomba
amewataka wahitimu kuendela kujifunza wawapo sehemu za kazi ili wawe
watendaji bora na kujiepusha na majanga ya utumiaji wa madawa ya
kulevya, ulevi na ukimwi ambavyo vina athiri wataalamu wengi hapa
nchini.
Ameongeza
kuwa Chuo hicho kina mpango wa kuanzisha mfumo wa uatamiaji wanafunzi
ili kuwawesha wahitimu kupata ajira mara wamalizapo masomo yao.
Kwa
upande wake Mkuu wa Chuo hicho Prof. Zacharia Mganilwa amesema idadi ya
Wanafunzi katika chuo hicho imeongeza kutoka 3500 mwaka 2014/15 hadi
kufikia 5340 mwaka huu na wahadhiri wameongezeka kutoka 63 mwaka 2012
hadi 167 mwaka 2017.
Zaidi ya
wanafunzi 1,029 wamehitimu Shahada ya Uzamili, Stashahada ya Uzamili,
Shahada na Diploma katika fani mbalimbali za usafirishaji na menejimenti
zitolewazo katika Chuo hicho.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: