CUF YALALAMIKIA 'WIZI' WA RUZUKU YAKE ; YAMTAKA RAIS MAGUFULI ACHUKUWE HATUA
Posted by khamisimussa77@gmail.com at 1:17 PM
Chama cha Wananchi (CUF) nchini Tanzania kimedai kuwa kimeibiwa fedha zake za Ruzuku kiasi cha shilingi milioni 369.
Akizungumza
mbele ya waandishi wa habari hii leo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi
wa chama hicho Julius Mtatiro amesema fedha hizo zilitoroshwa kutoka
Hazina ya Serikali Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania siku ya
Alhamisi, tarehe 5 ya mwezi huu wa Januari na kuingizwa kwenye akaunti
ya Benki ya NMB Tawi la Temeke, mjini Dar es Salaam.
Kwa
mujibu Mtatiro, fedha hizo zimehamishiwa kwenye akaunti ya mtu binafsi
aliye karibu na Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti taifa wa CUF
anayetambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa.
Amesema
CUF imeshangazwa na hatua hiyo kwa kuzingatia kuwa Msajili wa Vyama vya
Siasa Jaji Francis Mutungi alikiandikia barua chama hicho kukitaarifu
uamuzi wake wa kusimamisha mgao wake wa ruzuku kutokana na mgogoro wa
uongozi uliopo mpaka chama hicho kitakaporejea katika hali shwari
kiutendaji inayowezesha viongozi husika kusimamia matumizi ya fedha hizo
ipasavyo.
Kupitia taarifa hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya CUF mbali na
kushangazwa na hatua hiyo ya Hazina, amemtaka Rais Magufuli, Waziri
Mkuu Kasimu Majaliwa, Gavana wa Benki Kuu (BOT), TAKUKURU, Ofisi ya
Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali na vyombo vingine vinavyohusika,
kuchukua hatua za dharura za kuokoa fedha hizo za umma ambazo amesema,
zimepotezwa na watendaji wa Hazina kwa kuwa uhamishaji wake umefanyika
bila ya vyombo rasmi vya uongozi vya CUF na vinayotambulika kisheria
kuidhinisha suala hilo.
Chama
cha CUF kimetumbukia kwenye mgogoro mkubwa wa uongozi tangu mwenyekiti
wake Profesa Lipumba alipojiuzulu uongozi na kisha kubadilisha uamuzi
wake huo, hatua ambayo imepingwa na vyombo vya juu vya uongozi vya chama
hicho.
CUF inadai kuwa vyombo vya dola vya serikali ya chama tawala CCM vina mkono katika ''upikaji" wa mgogoro huo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: