ZA KIMATAIFA: HIMAYA YA UMOJA WA MATAIFA KWA JUHUDI ZA IRAN, RUSSIA NA UTURUKI ZA KUUPATIA UFUMBUZI MGOGORO WA SYRIA


Staffan de Mistura, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Syria amesema katika mazungumzo yake kwa njia ya simu na Sergey Lavrov, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Russia kwamba, anaunga mkono juhudi za Iran, Russia na Uturuki zenye lengo la kuupatia ufumbuzi mgogoro wa Syria.

Sergey Lavrov amesisitiza katika mazungumzo hayo juu ya natija ya kikao cha hivi karibuni cha Moscow, himaya na utayari wa Umoja wa Mataifa wa kusaidia kuandaa na kutekeleza hati ya makubaliano baina ya serikali na makundi ya upinzani yanayoipinga serikali ya Damascus kwa ajili ya kusitishwa mapigano nchini Syria na kuanza mazungumzo ya Wasyria kwa Wasyria katika mji mkuu wa Kazakhstan, Astana. 

Katika mazungumzo ya siku moja yaliyofanyika mjini Moscow tarehe 20 mwezi huu baina ya Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Russia na Uturuki, kulipasishwa taarifa ya pamoja iliyounga mkono juhudi za kuupatia ufumbuzi mgogoro wa Syria. Aidha kutakiwa jamii ya kimataifa kushirikiana katika vita dhidi ya ugaidi, kuhifadhiwa ardhi yote ya Syria, kukataliwa utumiaji wa nguvu za kijeshi katika kuutafuitia ufumbuzi mgogoro wa nchi hiyo, kutekelezwa azimio nambari 2254 la Umoja wa Mataifa, kupelekwa misaada ya kibinadanmu kwa Wasyria na kuondolewa raia katika maeneo yanayozingirwa na magaidi ni vipengee vingine vya taarifa ya kikao hicho cha Moscow.


Staffan de Mistura, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Syria

Kwa hakika matukio ya Syria katika miezi ya hivi karibuni yamebadilisha mahesabu ya makundi ya kigaidi na waungaji mkono wao. Katika fremu hiyo, kukombolewa mji muhimu na wa kiistartejia wa Halab kunahesabiwa kuwa nukta muhimu ya mafanikio katika vita dhidi ya ugaidi huko nchini Syria.  Ushindi huo wa Halab unatazamwa na Iran na Russia kuwa ni zaidi ya ushindani ulioko katika Mashariki ya Kati. Awali wakati wa kuanza machafuko nchini Syria, serikali ya Marekani ilikuwa ikiamini kwamba, kuangushwa serikali ya Rais Bashar al-Assad ni jambo lisiloepukika hata kidogo. Ni kwa msingi huo ndio maana Washington  kwa utendaji huo wa upande mmoja ikaiunga mkono Saudi Arabia, Uturuki, Qatar na makundi ya kigaidi huko Syria na ikayaimarisha na kuyapatia nguvu kwa kuyatumia silaha.

Sera za Saudi Arabia na Qatar za kuzusha migogoro pamoja na nafasi haribifu ya Marekani nchini Syria imepelekea kutokea maafa makubwa katika nchi hiyo. Washauri wa ikulu ya Marekani White House walikuwa wakidhani kwamba, kwa kuyaunga mkono makundi ya kigaidi na kuyagawa sehemu tatu za makundi mazuri, mabaya na ya wastani wangeweza kuhitimisha mara moja hatamu za serikali halali ya Syria chini ya uongozi wa Rais Assad.


Rais Bashar al-Assad wa Syria

Hata hivyo, kwenda kombo huko kimahesabu kumekuwa na taathira hasi mno. Kutokea maafa kama ya kuuawa kikatili wananchi wa Syria na makundi ya kigaidi ya Daesh na Jabh'hat al-Nusra, kuzingirwa miji kadhaa na kugeuzwa raia kuwa ngao  ya kujikingia na wakati huo huo kuongezeka wakimbizi ni matokeo ya utendaji wa kupenda vita nchini Syria ambapo nchi kama Uturuki nayo kwa siasa zake imechangia katika hilo.

Aidha serikali ya Marekani badala ya kurekebisha makosa yake, imeendelea kuyapatia misaada ya silaha makundi ya kigaidi nchini Syria.


Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran, Russia na Uturuki katika mkutano wao wa 20 Disemba mjini Moscow

Bashar al-Ja'far balozi na mwakilishi wa kudumu wa Syria katika Umoja wa Mataifa sambamba na kuashiria mgogoro wa kibinadamu ulioibuka nchini Syria kutokana na kuwepo magaidi katika nchi hiyo amesema kuwa, ili kuhitimisha mgogoro huo wa kibinadamu kuna haja ya kuweko ushirikiano na uratibu wa kimataifa na serikali ya Syria katika uwanja wa kupambana na ugaidi na wakati huo huo kutekelezwa maazimio ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika uwanja huo.

Hapana shaka kuwa, himaya ya Umoja wa Mataifa kwa juhudi za pamoja za Iran na Russia na matamshi ya Staffan de Mistura, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Syria kuhusiana na mwenendo chanya wa matukio ya nchi hiyo, ni jibu kwa propaganda na ukwamishaji mambo wa Marekani na Saudia baada ya kukombolewa mji wa Halab na kufanyika kikao cha pande tatu huko Moscow Russia.

0 comments: