Kiasi ya
watu sita wameuwawa na wengine 100 kujeruhiwa kufuatia shambulizi la
mabomu ya kutegwa ndani ya Lori lililofanywa na mshambuliaji wa kujitoa
muhanga mbele ya ubalozi mdogo wa Ujerumani, mjini Mazar-i-Shariff.
Kikundi
cha wapiganaji wa Taliban kimedai kuhusika na shambulizi hilo kwenye
ubalozi huo mdogo ulioko mji wa Mazar-i-Shariff, Kaskazini mwa
Afghanistan.
Wapiganaji
wa Taliban waliegesha lori lililokuwa na mabomu kwenye ukuta
unaozunguka ubalozi huo mdogo wa Ujerumani katika mji wa Mazar-i-Sharif,
jana usiku na kusababisha mauaji ya kiasi ya watu sita na wengine
wakajeruhiwa , maafisa wa Taliban wamesema.
Kufuatia
shambulizi hilo, waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Frank-Walter
Stainmeier ameitisha kikao na kikosi cha kukabiliana na majanga
kilichopo ndani ya wizara hiyo ili kwa pamoja kujadili hali ilivyo.
Msemaji
wa Gavana wa jimbo la Balkh, ambako kunapatikana ubalozi huo
aliyejulikana kwa jina moja, Munir amesema raia mmoja wa eneo
linapopatikana ubalozi aliripoti kusikia mripuko mkubwa uliofuatiwa na
milio ya risasi. Mripuko huo ndio uliosababisha kutawanyika kwa vigae
vya majengo yaliyoharibiwa yaliyokuwa jirani na ubalozi na kuwajeruhi
wengi.
Ofisi ya
mambo ya nje ya Ujerumani imeripoti shambulizi hilo kufanywa ndani na
nje ya ubalozi huo mdogo wa Ujerumani na kuongeza kuwa vikosi kutoka
Afghanistan na kikosi cha NATO walikuwepo kwenye tukio hilo. Vikosi
hivyo baadae viliripoti kumalizika kwa shambulizi hilo.
Maafisa
wa Afghanistan na madaktari wamesema zaidi ya watu 100 walijeruhiwa
kwenye shambulizi hilo. Mshambuliaji mmoja aliuwawa kwenye shambulizi.
Msemaji wa ofisi ya masuala ya nje ya Ujerumani amesema watumishi wote
wa ubalozi huo walikuwa salama na hawakudhurika na shambulizi hilo,
ingawa jengo la ubalozi liliharibiwa vibaya.
Mkuu wa
jeshi la polisi kwenye jimbo la Balkh ambako tukio hilo limetokea, Saied
Kamal amesema kulionekana mshambuliaji mmoja tu aliyehusika. Hata hivyo
baadae mamlaka zilieleza kumbaini mshambuliaji mwingine aliyefunikwa na
kifusi cha matofali. Ofisi ya masuala ya nje ya Ujerumani, iliripoti
kuzuiwa kwa washambuliaji hao na vikosi vya usalama, ingawa haikutaja
idadi yao halisi. Kiasi ya wanajeshi 900 wa Ujerumani walipelekwa eneo
hilo kuhakikisha usalama.
Kikundi
cha wapiganaji wa Taliban kimeeleza kuhusika na shambulizi hilo, kwa
madai ya kulipiza kisasi kufuatia shambulizi la anga lililofanywa
Novemba 3 na majeshi ya NATO karibu na Kaskazini mwa mji wa Kunduz na
kusababisha mauaji ya raia. Mapema mwezi huu, Jeshi la Marekani
lilieleza kuanzishwa kwa uchunguzi wa shambulizi hilo la anga ambalo
lilisababisha vifo na majeruhi kwa raia.
Maafisa
wa Taliban walisema, raia 33, ambao ni pamoja na watoto 17 walikufa
kufuatia shambulizi hilo la anga, na wengine 26 kujeruhiwa. jamaa ya
wahanga hao waliandamana hadi nje ya jengo la gavana wakilaani
shambulizi hilo. DW
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments: