MUUNGANO WA TANZANIA WAENDELEA KUIMARISHA UBORA WA ELIMU YA JUU

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano) Bi. Samia Suluhu Hassan (kulia) akimweleza jambo Afisa Habari Idara ya Habari (MAELEZO) Bi. Jovina Bujulu leo Mjini Dodoma.

Na Jovina Bujulu
Ubora wa elimu ya juu umeendelea kuimarika kwa kiasi kikubwa kutokana na kuwepo kwa Taasisi za muungano kama Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano) Bi. Samia Suluhu Hassan wakati wa mahojiano na Afisa Habari wa Idara ya Habari (MAELEZO) leo Mjini Dodoma.
Waziri Samia alisema kuwa kupitia Taasisi hizo wanafunzi wenye sifa kutpoka Tanzania Bara na Zanzibar wanapatiwa Mikopo ili kukidhi gharama za masomo.
“kumekuwepo na ushirikiano katika suala la elimu ya juu kwa mfano kati ya wanafunzi 600 kutoka zanzibar  wanaodahiliwa na Tume ya Vyuo vikuu Tanzania, 400 kati yao wanapatiwa mikopo na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ya Tanzania Bara na 200 waliosalia wanapatiwa mikopo na Bodi ya Mikopo ya ndani ya Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ” alisema Waziri Samia.
Akifafanua zaidi kuhusu umimarikaji wa Elimu ya Juu Waziri Samia alisema kuwa, Mwaka 1964, Zanzibar haikuwa na Chuo chochote cha Elimu ya Juu lakini kutokana na msisitizo uliowekwa katika kuiwezesha sekta hiyo Zanzibar imefanikiwa kuwa na vyuo vikuu 5.

Waziri Samia Alivitaja vyuo hivyo kuwa ni State University of Zanzibar (SUZA), Zanzibar University, Chuo cha Elimu cha Chukwani, chuo cha Afya na Chuo cha Fedha.
Serikali zitaendelea kuhakikisha kwamba nchi inaendelea kuwa yenye umoja, Amani , Utulivu na Usalama ili Muungano wetu uendelee kudumu na kuimarika kwa faida yetu na Vizazi Vijavyo

0 comments: